1Daudi akaondoka kule, akakimbilia kwenye pango karibu na muji wa Adulamu. Kaka zake na wandugu zake wengine waliposikia kwamba alikuwa pale, wote walikwenda kuungana naye.
2Watu wote waliogandamizwa au waliokuwa na madeni au wale wenye huzuni walijiunga na Daudi. Jumla yao ilikuwa watu yapata mia ine, naye akakuwa kiongozi wao.
3Kutoka kule, Daudi alikwenda mpaka Misipa katika inchi ya Moabu. Akamwambia mufalme wa Moabu: “Tafazali, baba yangu na mama yangu wakae hapa kwako mpaka nijue Mungu atanifanyia nini.”
4Basi, Daudi aliwaacha wazazi wake wakae na mufalme wa Moabu; nao wakakaa kwake kwa muda wote ambao Daudi alikuwa katika nafasi za makimbilio.
5Kisha nabii Gadi akamwambia Daudi: “Usikae hapa katika makimbilio. Ondoka mara moja uende katika inchi ya Yuda.” Basi, Daudi akaondoka, akaenda katika pori la Hereti.
6Siku moja, Saulo alikuwa Gibea, akiikaa chini ya muti wa mukwaju, kwenye mulima, naye alikuwa na mukuki wake katika mukono na watumishi wake walikuwa wakimuzunguka. Basi akaambiwa kwamba Daudi na watu wake wameonekana.
7Naye Saulo akawaambia watumishi wake: “Sasa ninyi watu wa kabila la Benjamina munisikilize, munazani kwamba huyu Daudi mwana wa Yese atamupa kila mumoja wenu mashamba ya mizabibu na mashamba mengine? Au munazani kwamba atamufanya kila mumoja wenu kuwa mukubwa wa waaskari maelfu au mukubwa wa waaskari mamia?
8Kwa nini ninyi wote mumenifanyia shauri baya? Hakuna hata mumoja wenu anayeniambia habari hii, wakati mwana wangu anapofanya mapatano na mutoto wa Yese. Tena, kwa nini hakuna hata mumoja kati yenu anayesikitika au kunielezea kwamba mwana wangu mwenyewe anamuchochea mutumishi wangu juu yangu akinivizia kama inavyokuwa leo hii?”
9Kwa hiyo Doegi Mwedomu, ambaye alikuwa amesimama karibu na watumishi wa Saulo akasema: “Nilimwona mwana wa Yese alipofika Noba kwa kuhani Ahimeleki mwana wa Ahitubu.
10Ahimeleki alimwombea Daudi kwa Yawe, akamupa chakula na upanga wa yule Mufilistini Goliati.”
11Mufalme Saulo akaagiza kuhani Ahimeleki mwana wa Ahitubu pamoja na watu wote wa jamaa ya baba yake ambao walikuwa makuhani kule Noba waitwe. Wote wakamwendea mufalme Saulo.
12Saulo akasema: “Sasa sikiliza wewe mwana wa Ahitubu.”
Ahimeleki akamujibu: “Ndiyo, bwana.”
13Saulo akamwambia: “Kwa nini wewe na Daudi mwana wa Yese, mumenifanyia shauri baya? Kwa nini ulimupatia mikate na upanga, halafu ukamwombea kwa Mungu? Kwa sababu hiyo, leo ameniasi na ananivizia.”
14Ahimeleki akamujibu: “Kati ya watumishi wako, Daudi ndiye mukubwa wa kuaminika kuliko wote. Yeye ni mukwe wako wewe mufalme mwenyewe, mukubwa wa waaskari wako walinzi na anaheshimiwa kuliko wote katika nyumba yako.
15Leo, sio mara ya kwanza kumwomba Mungu shauri kwa ajili yake. Mufalme, usiniwazie mimi wala mutu yeyote katika jamaa ya baba yangu juu ya mabaya yale. Mimi mutumishi wako, sijui neno lolote, likuwe kubwa au dogo juu ya jambo hilo.”
16Lakini mufalme Saulo akamwambia: “Ahimeleki, hakika utauawa, wewe na jamaa yote ya baba yako.”
17Saulo akawaambia walinzi waliokuwa wakisimama pembeni yake: “Mugeuke na kuwaua makuhani wa Yawe, maana wao wanapatana na Daudi; walijua kwamba ametukimbia wala hawakuniarifu.” Lakini walinzi hao hawakuinua mikono yao kwa kuwaua makuhani wa Yawe.
18Kwa hiyo, mufalme Saulo akamwambia Doegi: “Wewe geuka uwaue makuhani.” Doegi Mwedomu akaenda na kuwaua makuhani wote. Siku hiyo, Doegi aliua makuhani makumi nane na watano ambao wanavaa vizibao vya kikuhani vya kitani.
19Kisha aliwaua kwa makali ya upanga wakaaji wote wa Noba, muji wa makuhani, wanaume na wanawake, watoto wadogo na wenye kunyonya, ngombe, punda na kondoo.
20Lakini Abiatari, mumoja wa watoto wa kiume wa Ahimeleki mwana wa Ahitubu, aliponyoka akakimbilia kwa Daudi.
21Abiatari alimwelezea Daudi kwamba Saulo amewaua makuhani wa Yawe.
22Naye Daudi akamwambia Abiatari: “Nilijua wazi siku ile nilipomwona Doegi Mwedomu, kwamba atamwambia Saulo. Kwa hiyo mimi nimesababisha vifo vya watu wa jamaa ya baba yako.
23Wewe, ukae pamoja nami, wala usiogope. Maana, anayetafuta kuyaangamiza maisha yangu anatafuta hata yako vilevile. Ukiwa pamoja nami, uko salama kabisa.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.