Isaya 66 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Ibada ya uongo na ya kweli

1Yawe anasema hivi:

Mbingu ni kiti changu cha kifalme,

dunia ni kiti cha kupumzikishia miguu yangu.

Mutanijengea nyumba ya namna gani basi,

pahali nitakapoweza kupumzikia?

2Mimi mwenyewe nilivifanya vitu hivi vyote,

na hivi vyote ni mali yangu.

Lakini ninachojali mimi,

ni mutu munyenyekevu na mwenye moyo wenye kuvunjika,

mutu anayetetemeka anaposikia neno langu.

–Ni ujumbe wa Yawe.

3Lakini watu hawa wanafanya wanavyotaka:

wananitolea sadaka ya ngombe

na tena wanaua watu kwa kutambikia.

Wananitolea sadaka ya mwana-kondoo

na vilevile wanaua imbwa.

Wananitolea sadaka ya unga

na vilevile wanatolea damu ya nguruwe.

Wanachoma ubani mbele yangu

na kwenda kuabudu miungu ya uongo.

Hao wamechagua kufuata njia zao wenyewe.

4Basi, nitawaletea taabu;

zile hasara zote wanazoogopa zitawapata;

maana nilipoita hakuna aliyeitika,

niliposema hawakunisikiliza.

Lakini walifanya maovu mbele yangu,

walichagua yale ambayo hayanipendezi.

Azabu na wokovu

5Musikilize neno la Yawe,

enyi munaotetemeka kwa sababu ya neno lake.

Wandugu zenu ambao wanawachukia,

na kuwafukuza kwa sababu yangu,

wamesema hivi kwa kuwachekelea:

Mungu aonyeshe utukufu wake,

nasi tuwaone ninyi mukishinda!

Lakini wao wenyewe ndio watakaopata haya!

6Musikilize: makelele kutoka katika muji,

sauti kutoka katika hekalu!

Hiyo ni sauti ya Yawe

akiwaazibu waadui zake!

7Muji wangu mutakatifu,

ni kama mama anayezaa bila kupata uchungu;

mbele ya uchungu kuanza, amekwisha zaa mutoto.

8Ni nani aliyepata kusikia jambo kama lile?

Ni nani aliyepata kuona jambo kama lile?

Inchi nzima inaweza kuzaliwa kwa siku moja?

Taifa zima linaweza kuzaliwa kwa mara moja?

Maana mara moja tu Sayuni ulipoanza kupata uchungu,

palepale ukazaa watoto wake.

9Namna gani ninaweza kumufikisha mutoto kwa saa ya kuzaliwa,

halafu nimuzuize asizaliwe?

–Ni Yawe anayesema hivyo.–

Au mimi mwenye kuwajalia watoto,

namna gani nitafunga uzazi?

–Ni Mungu wenu anayesema hivyo.

10Mushangilie na kufurahi pamoja na Yerusalema, enyi munaoupenda!

Mushangilie pamoja nao, enyi wote mulioulilia!

11Hivi mutapata kunyonya,

nanyi mutashiba kwa riziki zake;

mutayakunywa na kufurahi,

kutokana na wingi wa utukufu wake.

12Maana Yawe anasema hivi:

Nitakuletea fanaka nyingi kama muto,

utajiri wa mataifa kama muto uliofurika.

Nanyi mutanyonya na kubebwa kama mutoto muchanga,

mutabembelezwa kama mutoto juu ya magoti ya mama yake.

13Kama vile mama anavyomufariji mwana wake,

vilevile nami nitawafariji;

mutafarijiwa katika Yerusalema.

14Mutayaona hayo na mioyo yenu itafurahi;

mifupa yenu itastawi tena kama vile majani mabichi.

Kwa hiyo itajulikana kwamba mimi Yawe

ninawalinda watumishi wangu,

lakini nikikasirika ninawaazibu waadui zangu.

15Yawe atakuja kama moto,

na magari yake ya vita ni kama zoruba.

Ataiacha hasira yake ifanye kazi yake kwa ukali,

na maonyo yake yatimizwe kwa ndimi za moto.

16Yawe atatoa hukumu kwa moto

atawaazibu watu wote kwa upanga;

nao atakaowaangamiza watakuwa wengi.

17Kuna watu wanaojitakasa na kujisafisha wapate kuingia kwenye bustani za ibada za sanamu; wanafanya maandamano na kuhani akiwa kati yao. Watu wale wanakula nguruwe, panya na vyakula vingine vyenye kuwa machukizo. Watu wale hakika watakufa wote pamoja.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Ulimwengu mupya

18Ninayajua matendo yao na mawazo yao. Ninakuja kuwakusanya watu wa mataifa yote na wa luga zote, wakusanyike pamoja na kuuona utukufu wangu.

19Nitaweka kati yao kitambulisho cha uwezo wangu. Watakaookolewa kati yao nitawapeleka kwa watu wa mataifa kule Tarsisi, Puti, Ludi, inchi zenye wafundi wa kupiga upinde; watakwenda vilevile Tubali na Ugriki na katika visanga vya mbali ambapo watu hawajapata kusikia habari zangu wala kuuona utukufu wangu. Wale wajumbe wangu watautangaza utukufu wangu katika mataifa hayo.

20Watawarudisha wandugu zenu wote kutoka katika mataifa yote kama matoleo yangu mimi Yawe. Watawaleta juu ya farasi, juu ya nyumbu, juu ya ngamia na ndani ya magari na juu ya vipoyi mpaka Yerusalema, kwenye mulima wangu mutakatifu. Watawaleta kama Waisraeli wanavyoleta sadaka ya unga katika chombo safi mpaka ndani ya nyumba yangu mimi Yawe.

21Vilevile nitawachagua wamoja kati yao kuwa makuhani na Walawi. –Ni Yawe anayesema hivyo.

22Kama vile mbingu mupya na dunia mupya nitakazoumba

zitakavyodumu milele kwa uwezo wangu,

ndivyo wazao wako na jina lako litakavyodumu.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

23Katika kila sikukuu ya mwandamo wa mwezi,

na katika kila siku ya Sabato,

wanadamu wote watakuja kuniabudu.

–Ni Yawe anayesema hivyo.

24Kisha watakwenda kuziona maiti za wale walioniasi. Wadudu watakaowakula hawatakufa, na moto utakaowachoma hautazimika hata kidogo. Watakuwa chukizo kwa watu wote.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help