Marko 1 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mahubiri ya Yoane Mubatizaji(Mat 3.1-12; Lk 3.1-18; Yn 1.19-28)

1Huu ndio mwanzo wa Habari Njema ya Yesu Kristo, Mwana wa Mungu.

2Na imeandikwa hivi katika kitabu cha nabii Isaya:

“Mungu anasema:

‘Ninamutuma mujumbe wangu akutangulie,

kusudi akutengenezee njia.’

3Sauti inatangaza katika jangwa:

‘Mutengeneze njia ya Bwana,

munyooshe pahali atakapopita!’ ”

4Hivi Yoane alitokea katika jangwa, akibatiza watu, akiwahubiri kwamba wageuke toka zambi zao, wabatizwe, na Mungu atawasamehe.

5Watu wengi walitoka katika Yerusalema na katika jimbo lote la Yudea kwa kumwendea Yoane. Walikubali zambi zao, naye akawabatiza katika muto Yordani.

6Yoane alikuwa akivaa nguo iliyotengenezwa na manyoya ya ngamia na mukaba wa ngozi katika kiuno. Naye alikuwa akikula nzige na asali ya pori.

7Yeye alihubiri hivi kwa watu: “Yule anayekuja nyuma yangu ni mwenye uwezo kunipita; nami sistahili hata kuinama na kufungua kamba ya viatu vyake.

8Mimi nimewabatiza kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa Roho Mutakatifu.”

Ubatizo wa Yesu na kujariba kwake(Mat 3.13–4.11; Lk 3.21-22; 4.1-13)

9Katika siku zile, Yesu akatoka Nazareti, katika Galilaya, akabatizwa na Yoane katika Yordani.

10Mara moja wakati Yesu alipotoka ndani ya maji, akaona mbingu zinafunguka na Roho Mutakatifu akishuka juu yake kwa mufano wa njiwa.

11Na sauti ikasikilika toka mbinguni, ikisema: “Wewe ndiwe Mwana wangu mupendwa; ninapendezwa nawe sana.”

12Kisha Roho Mutakatifu akamusukuma Yesu kwenda katika jangwa.

13Akabaki katika jangwa kwa muda wa siku makumi ine, na kule Shetani akamujaribu. Alikaa kule katikati ya nyama wa pori, nao wamalaika walimushugulikia.

Yesu anaita wanafunzi wa kwanza(Mat 4.12-22; Lk 4.14-15; 5.1-11)

14Nyuma ya kutiwa kwa Yoane katika kifungo, Yesu alikwenda Galilaya, akahubiri Habari Njema inayotoka kwa Mungu.

15Alisema: “Wakati umetimia, na Ufalme wa Mungu ni karibu! Mugeuke toka zambi zenu na kukubali Habari Njema!”

16Wakati Yesu alipokuwa akitembea pembeni ya ziwa la Galilaya akawaona wavuvi wawili, waliokuwa wandugu za tumbo: Simoni na ndugu yake Andrea. Walikuwa wakitupa nyavu katika ziwa lile.

17Yesu akawaambia: “Munifuate, nami nitawaweka kwa kazi ya kuopoa watu.”

18Mara moja wakaacha nyavu zao na kumufuata.

19Yesu alipoendelea mbele kidogo, akawaona wandugu wengine wawili: Yakobo na Yoane waliokuwa wana wa Zebedayo. Walikuwa ndani ya chombo wakitengeneza nyavu zao.

20Mara moja akawaita. Basi wakamwacha baba yao Zebedayo ndani ya chombo pamoja na watumishi wake, wakamufuata Yesu.

Yesu anaponyesha mutu mwenye pepo(Lk 4.31-37)

21Yesu na wanafunzi wake walienda Kapernaumu. Siku ya Sabato ilipotimia, Yesu akaingia katika nyumba ya kuabudia na kufundisha watu.

22Watu waliomusikia walishangaa sana kuona namna alivyofundisha, kwa maana hakuwafundisha sawa na walimu wao wa Sheria, lakini kama mutu mwenye mamlaka.

23Saa ile, mutu mumoja aliyeshikwa na pepo alikuwa ndani ya nyumba ya kuabudia. Akaanza kulalamika, akisema:

24“Kuna maneno gani kati yako na sisi, wewe Yesu wa Nazareti? Ulikuja kutuangamiza? Ninakutambua wewe ni nani: wewe ni Mutakatifu aliyetumwa na Mungu.”

25Yesu akamukaripia kwa nguvu, akimwamuru: “Nyamaza, na utoke ndani ya mutu huyu!”

26Yule pepo akamutikisa mutu yule kwa nguvu, akatoka ndani yake, akilalamika kwa nguvu.

27Watu wote wakashangaa sana na kuulizana: “Hatujaona mambo kama haya! Hakika mafundisho haya ni yenye mamlaka! Mutu huyu anaamuru hata pepo, nao wanamutii!”

28Halafu sifa za Yesu zikaenea upesi katika jimbo lote la Galilaya.

Yesu anaponyesha wagonjwa wengi(Mat 8.14-17; Lk 4.38-41)

29Yesu na wanafunzi wake walipotoka ndani ya ile nyumba ya kuabudia, mara moja wakaenda kwa nyumba ya Simoni na Andrea, wakiwa pamoja na Yakobo na Yoane.

30Mama mukwe wa Simoni alikuwa katika kitanda, kwa sababu alikuwa na homa. Wakati Yesu alipofika pale, mara moja wakamupasha habari ya ugonjwa wake.

31Basi Yesu akajongea karibu naye, akamushika mukono na kumusimamisha. Naye akapona homa na kuanza kuwashugulikia.

32Ilipokuwa magaribi, jua lilipokuwa limekwisha kutua, wakamuletea Yesu watu wote waliokuwa wagonjwa na waliokuwa na pepo.

33Watu wote wa muji walikusanyika mbele ya mulango wa nyumba.

34Yesu akawaponyesha watu wengi wenye magonjwa mbalimbali. Vilevile alifukuza pepo wengi, wala hakuwaachilia pepo kusema neno, kwa sababu walimujua yeye ni nani.

Yesu anahubiri katika Galilaya(Lk 4.42-44)

35Kesho yake asubui kulipokuwa kungali giza, Yesu akaamuka, akatoka katika muji na kwenda pahali penye ukiwa, kule akaanza kuomba.

36Basi Simoni na wenzake wakaenda kumutafuta.

37Nao walipomwona wakamwambia: “Watu wote wanakutafuta.”

38Lakini Yesu akawajibu: “Twende pahali pengine katika vijiji vinavyokuwa karibu, kusudi nihubiri kule vilevile, kwa maana ni kwa ajili ya ile nimekuja.”

39Hivi akaenda fasi zote katika Galilaya, akihubiri katika nyumba za kuabudia na kufukuza pepo.

Yesu anaponyesha mwenye ukoma(Mat 8.1-4; Lk 5.12-16)

40Mutu mumoja mwenye ukoma alikuja kwa Yesu, akapiga magoti mbele yake na kumusihi, akisema: “Kama ukitaka, unaweza kunitakasa.”

41Yesu akamusikilia huruma, akanyoosha mukono, akamugusa na kumwambia: “Ninataka utakaswe!”

42Na mara moja mutu yule akapona ukoma na kutakaswa.

43Pale pale Yesu akamwagiza kwa nguvu aende na kusema:

44“Angalisho, usimwambie mutu hata neno moja juu ya hii. Lakini kwenda kwa kuhani na kumwonyesha jinsi unavyokuwa sasa. Kisha utoe sadaka kama Musa alivyoamuru, kuwa ushuhuda kwa wote kwamba umetakaswa.”

45Lakini mutu yule alipoenda, akaanza kutangaza habari zile fasi zote. Na kwa sababu hii Yesu hakuweza kuingia tena waziwazi katika muji wowote, lakini alibaki mbali nayo pahali penye ukiwa. Na watu walimufikia kule kutoka pande zote.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help