Yobu 1 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Shetani amujaribu Yobu

1Kulikuwa mutu mumoja katika inchi ya Usi, aliyeitwa Yobu. Mutu yule alikuwa mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu.

2Yobu alikuwa na wana saba na wabinti watatu.

3Alikuwa na mali, kondoo elfu saba, ngamia elfu tatu, ngombe elfu moja, punda dike mia tano, na watumishi wengi sana. Yeye alikuwa wa heshima kuliko watu wote kule upande wa mashariki.

4Mara kwa mara, wana wa Yobu walifanya karamu katika nyumba ya kila mumoja wakifuatana. Waliwaalika wadada zao kula na kunywa pamoja nao.

5Kila mara karamu ilipomalizika, Yobu aliita wana wake kusudi awatakase. Aliamuka asubui mapema kisha karamu, akatoa sadaka za kuteketezwa kwa moto kwa ajili ya kila mumoja wao maana aliwaza: “Labda wana wangu wametenda zambi na kumutukana Mungu ndani ya mioyo yao.”

6Basi, ikatukia siku moja wamalaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Yawe. Shetani akakuja kuwa pamoja nao.

7Yawe akamwuliza Shetani: “Unatoka wapi wewe?”

Shetani akamujibu Yawe: “Ninatoka kutembeatembea na kuzungukazunguka katika dunia.”

8Yawe akamwambia Shetani: “Umemwona vizuri mutumishi wangu Yobu? Katika dunia hakuna mwingine anayekuwa kama yeye. Yeye ni mutu mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu.”

9Shetani akamujibu Yawe: “Yobu anamwogopa Yawe kwa bure? Ang. Ufu 12.10

10Si wewe mwenyewe unamulinda pande zote pamoja na jamaa yake na kila kitu anachokuwa nacho? Wewe umemubariki na mali yake imeongezeka katika inchi.

11Lakini sasa, unyooshe mukono wako uguse mali yake. Utaona namna atakutukana waziwazi!”

12Yawe akamwambia Shetani: “Basi, unaweza kufanya vile unavyotaka juu ya mali yake. Lakini tu yeye mwenyewe usimuguse.” Basi, Shetani akaondoka mbele ya Yawe.

Jaribu la kwanza la Yobu

13Siku moja, wana na wabinti wa Yobu walikuwa wanakula na kunywa divai pamoja katika nyumba ya kaka yao mukubwa.

14Basi, mutumishi akafika kwa Yobu, akamwambia: “Tulikuwa tunalima kwa majembe ya kukokotwa na ngombe. Punda nao walikuwa wanakula pale karibu.

15Basi Wasabea wakatushambulia na kunyanganya nyama na kuua watumishi kwa upanga. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.”

16Alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akafika, akasema: “Umeme wa radi umewachoma na kuwateketeza kondoo na watumishi. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.”

17Yule naye alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akafika, akasema: “Wakaldea walijipanga makundi matatu, wakashambulia ngamia, wakawatwaa, na wakaua watumishi wako kwa upanga! Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.”

18Alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akakuja, akasema: “Wana zako na wabinti zako walikuwa wanakula na kunywa divai katika nyumba ya kwa kaka yao mukubwa.

19Mara moja upepo mukali ukavuma kutoka katika jangwa, ukaipiga nyumba ile kila upande nayo ikawaangukia, na vijana wote wamekufa. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.”

20Kisha Yobu akasimama, akapasua nguo yake, akanyoa nywele zake, akajitupa chini na kumwabudu Mungu,

21akisema:

Nilikuja uchi katika dunia,

nitaondoka uchi katika dunia.

Yawe amenipa,

Yawe ametwaa.

Jina la Yawe litukuzwe.

22Katika mambo haya yote Yobu hakutenda zambi wala hakumushitaki Mungu kuwa na kosa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help