Nehemia 3 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Ukuta wa Yerusalema unajengwa upya

1Basi Eliasubu, Kuhani Mukubwa, pamoja na wandugu zake waliokuwa makuhani wakasimama na kuanza kujenga Mulango wa kondoo. Wakautakasa na kutia milango yake; wakaitakasa tangia kwenye Munara wa Mia Moja mpaka Munara wa Hananeli.

2Sehemu iliyofuata ilijengwa upya na watu wa muji wa Yeriko. Nyuma ya hayo aliyefuata ni Zakuri mwana wa Imuri kwa kujenga sehemu ya ukuta.

3Nao watu wa ukoo wa Hasena wakajenga upya Mulango wa Samaki, wakatia miimo yake, milango, vyuma na vifungio vyake.

4Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Meremoti mwana wa Uria, mujukuu wa Hakosi. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Mesulamu mwana wa Berekia, mujukuu wa Mesezabeli. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Zadoki mwana wa Bana.

5Sehemu inayofuata ikajengwa na watu kutoka muji wa Tekoa. Lakini viongozi wa muji wakakataa kufanya kazi ya mikono waliyoagizwa kufanya na wasimamizi.

6Mulango wa zamani; ukajengwa upya na Yoyada mwana wa Pasea, pamoja na Mesulamu mwana wa Besodia, wakatia miimo yake, milango, vyuma na vifungio vyake.

7Waliowafuata hao katika kazi hiyo ya kujenga upya walikuwa Melatia, Mugibeoni; Yadoni, Mumeronoti pamoja na watu wa muji wa Gibeoni na Misipa waliokuwa chini ya uongozi wa mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati.

8Sehemu inayofuata, ilijengwa upya na Usieli mwana wa Harihaya, mufua zahabu. Sehemu inayofuata mpaka kwenye Ukuta Mupana ikajengwa upya na Hanania, mutengenezaji wa marasi.

9Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Refaya mwana wa Huri, mukubwa wa nusu ya wilaya ya Yerusalema.

10Sehemu inayofuata, inayoelekeana na nyumba yake ikajengwa upya na Yedaya mwana wa Harumafu. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Hatusi mwana wa Hasabunia.

11Sehemu inayofuata pamoja na Munara wa Furu vilijengwa upya na Malkiya, mwana wa Harimu akishirikiana na Hasubu mwana wa Pahati-Moabu.

12Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Salumu mwana wa Halohesi, mutawala wa nusu nyingine ya wilaya ya Yerusalema. Alisaidiana na binti zake katika ujenzi huo.

13Mulango wa Bonde ukajengwa upya na Hanuni pamoja na wakaaji wa muji wa Zanoa. Wakaweka milango pahali pake, wakatia vyuma na vifungio vyake. Wakajenga upya ukuta ukiwa na urefu wa metre mia ine hivi mpaka kwenye mulango wa Yalala.

14Mulango wa Yalala ukajengwa upya na Malkiya mwana wa Rekabu, mukubwa wa wilaya ya Beti-Hakeremu. Akaweka mulango kwa nafasi yake, akatia vyuma na vifungio vyake.

15Mulango wa Chemichemi ukajengwa upya na Salumu mwana wa Koli-Hoze, mukubwa wa wilaya ya Misipa. Akaufunika, akauweka mulango kwa nafasi yake, akatia vyuma na vifungio vyake. Kwenye Kisima cha Sela akajenga ukuta unaokuwa karibu na bustani ya kifalme mpaka kwenye ngazi zinazoshuka toka muji wa mufalme Daudi.

16Sehemu inayofuata mpaka kwenye makaburi ya Daudi, kisima na majengo ya waaskari ikajengwa upya na Nehemia mwana wa Aibuki, mukubwa wa nusu ya wilaya ya Beti-Suri.

Walawi waliojenga ukuta

17Nyuma ya hao, Walawi waliendelesha ujenzi mupya wa ukuta. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Rehumu mwana wa Bani, na Hasabia, mutawala wa nusu ya wilaya ya Keila, akajenga upya sehemu ya upande wa wilaya yake.

18Nyuma yake, sehemu zinazofuata zikajengwa upya na wandugu zao. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Bawayi mwana wa Henadadi, mutawala wa nusu ya wilaya ya Keila.

19Sehemu inayofuata inayoelekeana na gala ya silaha kwenye pembe ya ukuta ikajengwa upya na Ezeri mwana wa Yesua, mutawala wa Misipa.

20Sehemu inayofuata tangia kwenye pembe mpaka kwenye mulango wa Eliasibu, Kuhani Mukubwa, ikajengwa upya na Baruku mwana wa Zabayi.

21Sehemu inayofuata tangia kwenye mulango wa nyumba ya Eliasibu, Kuhani Mukubwa, mpaka mwisho wa nyumba hiyo, ikajengwa upya na Meremoti mwana wa Uria, mujukuu wa Hakosi.

Makuhani waliojenga ukuta

22Sehemu inayofuata ikajengwa upya na makuhani waliokaa katika sehemu ya mabonde.

23Benjamina na Hasubu wakajenga upya sehemu inayoelekeana na nyumba yao. Azaria mwana wa Masea, mujukuu wa Anania, akajenga upya sehemu inayoelekeana na nyumba yao.

24Kuanzia kwenye nyumba ya Azaria mpaka kwenye pembe ya ukuta ikajengwa upya na Binui mwana wa Henadadi.

25Sehemu inayofuata, tokea kwenye pembe ya ukuta na munara wa nyumba ya kifalme ya juu karibu na kiwanja cha walinzi ikajengwa upya na Palali mwana wa Uzayi. Pedaya mwana wa Parosi,

26akishirikiana na watumishi wa hekalu waliokaa Ofeli, wakajenga upya sehemu inayoelekeana na Mulango wa Maji, upande wa mashariki na munara murefu.

Wajengaji wengine

27Sehemu ingine inayofuata, ikitokea kwenye munara murefu mpaka kwenye ukuta wa Ofeli ikajengwa upya na wakaaji wa muji wa Tekoa.

28Juu ya Mulango wa Farasi kulikuwa kundi la makuhani, kila mumoja akajenga sehemu inayoelekeana na nyumba yake.

29Zadoki mwana wa Imeri akajenga upya sehemu inayoelekeana na nyumba yake. Sehemu inayofuata, ikajengwa upya na Semaya mwana wa Sekania, mulinzi wa Mulango wa Mashariki,

30Sehemu inayofuata ikiwa ni sehemu yao ya pili ikajengwa upya na Hanania mwana wa Selemia, akishirikiana na Hanuni mwana wa sita wa Zalafi. Mesulamu mwana wa Berekia, akajenga upya sehemu inayoelekeana na chumba chake.

31Sehemu inayofuata, tokea kwenye nyumba ya watumishi wa hekalu na wachuuzi iliyokuwa inaelekeana na Mulango wa Gereza, karibu na chumba cha juu kwenye pembe upande wa kaskazini-mashariki ikajengwa upya na Malkiya, mufua zahabu.

32Sehemu ya mwisho kutokea kwa chumba kwenye pembe mpaka kwenye Mulango wa Kondoo ikajengwa upya na wafua zahabu na wachuuzi.

Nehemia anashinda upinzani

33Sanibalati aliposikia kwamba tumeanza kazi ya kuujenga upya ukuta akakasirika sana, akaanza kutuchekelea

34mbele ya warafiki zake na waaskari wa Wasamaria, akisema: “Hawa Wayuda wasiokuwa na nguvu wanafanya nini? Kusudi lao ni kuujenga upya muji? Watatoa sadaka? Wanaweza kumaliza kazi kwa siku moja tu? Wataweza kufanya mawe yaliyolundikana kwenye takataka na yaliyochomwa yakuwe ya kujenga?”

35Tobia, Mwamoni, aliyekuwa akisimama karibu naye, akatilia mukazo akisema: “Wanajenga nini? Mbweha akipanda juu yake, atabomoa ule ukuta wao wa mawe!”

36Halafu nikamwomba Mungu nikisema: “Ee Mungu wetu, sikia namna wanavyotuchekelea; urudishe mazarau yao juu yao wenyewe. Uwaache watekwe na kupelekwa katika inchi ya kigeni.

37Usiwasamehe makosa yao hata kidogo, wala zambi yao usiisamehe hata kidogo; maana wamekukasirikisha mbele ya wajengaji.”

38Lakini tukaendelea na ujenzi wa ukuta mpaka ukafikia nusu yake kwa sababu watu walikuwa wakitumika kwa bidii.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help