Yobu 34 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kisha Elihu akaendelea kusema:

2Musikilize maneno yangu, enyi wenye hekima,

munitegee masikio yenu, ninyi wenye ujuzi.

3Sikio linapima maneno,

kama vile ulimi unavyoonja chakula.

4Basi, tuchague sasa yanayokuwa sawa,

tuamue kati yetu yanayokuwa mazuri.

5Basi, Yobu amesema: “Mimi Yobu sina kosa,

Mungu ameniondolea haki yangu.

6Ingawa sina kosa, ninaonekana kuwa mwongo.

Kidonda changu hakiponi ingawa sina kosa.”

7Ni nani anayekuwa kama Yobu

ambaye kwake mazarau ni kama kunywa maji?

8Anaandamana na watenda maovu,

anatembea na watu waovu.

9Maana amesema: “Mutu hapati faida yoyote

na kujisumbua kumupendeza Mungu.”

10Kwa hiyo munisikilize, enyi wenye ujuzi.

Mungu hawezi kufanya uovu hata kidogo;

Mungu Mwenye Uwezo hawezi kufanya kosa.

11Mungu atamulipa mutu kadiri ya matendo yake,

atamulipiza kulingana na mwenendo wake.

12Ni ukweli mutupu: Mungu hafanyi jambo ovu.

Mungu Mwenye Uwezo hapotoshi haki hata kidogo.

13Kuna yule aliyemupatia mamlaka juu ya dunia?

Uwezo wake juu ya ulimwengu ni wake peke yake.

14Kama Mungu angejifikiri tu yeye mwenyewe,

akiondoa pumzi yake ya uzima katika dunia,

15viumbe vyote vingeangamia kabisa,

naye mwanadamu angerudi katika mavumbi.

16Kama una akili sikiliza;

sikiliza ninachokuambia.

17Anayetawala ulimwengu kwa sheria zake anachukia haki?

Utasubutu kumuhukumu mwenye haki na mwenye nguvu,

18anayemwambia mufalme “Wewe ni wa ovyo!”

na watu wenye heshima “Ninyi ni waovu!”

19Yeye hawapendelei wakubwa,

wala kuwajali watajiri kuliko wamasikini,

maana wote hao ni kazi ya mikono yake.

20Kufumba na kufumbua hao wamekufa;

wanatikiswa usiku na kuaga dunia;

nao wenye nguvu wanaondolewa bila kutumia nguvu za mutu.

21Macho ya Mungu yanachunguza mienendo ya watu;

yeye anaziona hatua zao zote.

22Hakuna weusi wala giza kubwa

ambamo watenda maovu wanaweza kujificha.

23Mungu hahitaji kumujulisha mutu

wakati wa kumuleta mbele ya tribinali yake.

24Anawaangamiza wenye nguvu bila uchunguzi,

na kuwaweka wengine pahali pao.

25Kwa maana anayajua matendo yao yote,

anawapindua usiku waangamie.

26Anawapiga mbele ya watu kwa ajili ya uovu wao,

27kwa sababu wameacha kumufuata yeye,

wakazarau njia zake zote.

28Hata wakasababisha kilio cha wamasikini kimufikie Mungu.

Mungu akasikiliza kilio cha wale walioteswa.

29Kama Mungu akinyamaza, nani anayeweza kumuhukumu?

Kama akificha uso wake, nani anayeweza kumwona,

ikiwa ni taifa au mutu mumoja?

30Anafanya hivyo, mutu mubaya asitawale,

au wale wanaohatarisha maisha ya watu.

31Labda mutu atamwambia Mungu hivi:

“Nimekosa, sitatenda zambi tena.

32Unionyeshe makosa nisiyoweza kuyaona.

Kama nimetenda mabaya, sitayarudilia tena.”

33Mungu atapaswa kumwazibu kama unavyoona wewe?

Wewe ndiwe unayeamua, wala si mimi.

Basi, sema unachofikiri wewe.

34Mutu yeyote mwenye akili,

na kila mwenye hekima anayenisikiliza atasema:

35“Yobu anaongea bila kutumia akili,

maneno yake hayana maana.”

36Heri Yobu angechunguzwa mpaka mwisho,

kwa maana anajibu kama watu waovu.

37Anaongeza uasi juu ya zambi zake;

anaeneza mashaka kati yetu,

na kuzidisha maneno yake juu ya Mungu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help