Isaya 52 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu atakomboa Yerusalema

1Amuka! Amuka!

Ujipatie zile nguvu zako, ewe Sayuni!

Uvae nguo yako nzuri,

ewe Yerusalema, muji mutakatifu.

Maana hawataingia tena kwako

watu wasiotahiriwa na wachafu.

2Ujikungute mavumbi, usimame,

ewe Yerusalema uliyekuwa mufungwa!

Ujifungue minyororo yako katika shingo,

ewe binti Sayuni uliyekamatwa mateka.

3Yawe anasema hivi: Ninyi muliuzishwa bure bila malipo yoyote, na mutakombolewa bila kulipa feza.

4Tena zamani ninyi watu wangu mulikimbilia Misri mukakaa kule. Halafu nyuma Waasuria waliwagandamiza bila sababu yoyote.

5Katika hali ya sasa ninapata faida gani kuwaona watu wangu wamepelekwa katika utumwa? –Ni ujumbe wa Yawe.

Hao wanaowatawala wanajitapa. Nalo jina langu linaendelea kuzarauliwa kila siku. –Ni ujumbe wa Yawe.

6Kwa hiyo watu wangu watajua mimi ni nani. Siku hiyo watajua kwamba ni mimi ninayesema: “Niko!”

7Ni furaha kabisa!

Mujumbe anatokea kwenye mulima.

Anatangaza habari njema

za amani, heri, na ukombozi.

Anauambia Sayuni:

Mungu wako anatawala!

8Sikiliza sauti ya walinzi wako;

wanaimba pamoja kwa furaha,

maana wanaona kwa macho yao wenyewe

kurudi kwa Yawe katika Sayuni.

9Mupige kelele za shangwe, enyi mabomoko ya Yerusalema!

Yawe amewafariji watu wake,

ameukomboa Yerusalema.

10Yawe ameonyesha nguvu yake tukufu,

mbele ya mataifa yote.

Atawaokoa watu wake,

na ulimwengu wote utashuhudia.

11Muondoke! Muondoke! Mutoke pale!

Musiguse kitu chochote kichafu!

Muondoke kule Babeli!

Mujitakase, enyi munaobeba vyombo vya Yawe.

12Mara hii hamutatoka kwa haraka,

wala hamutaondoka mbiombio!

Maana Yawe atawatangulia,

Mungu wa Israeli atawalinda nyuma yenu.

Mutumishi wa Yawe

13Mungu anasema hivi:

Mutumishi wangu atafanikiwa;

atatukuzwa na kupewa cheo,

atapata heshima kubwa.

14Wengi waliomwona walishituka,

kwa vile sura yake ilikuwa imeharibika;

hakukuwa tena na umbo la mwanadamu!

15Lakini sasa ameyashangaza mataifa mengi.

Wafalme watapumbazika kwa sababu yake,

maana wataona mambo ambayo hawajapata kuambiwa,

na kufahamu mambo ambayo hawajapata kusikia.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help