Esteri 3 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Hamani anafanya shauri la kuwaangamiza Wayuda

1Nyuma ya mambo hayo, mufalme Ahasuero akamupandisha Hamani cheo, akakuwa waziri mukubwa. Hamani alikuwa mwana wa Hamedata wa uzao wa Agagi.

2Mufalme akaamuru wakubwa wote wa serikali yake wamutii Hamani kwa kuinama na kupiga magoti mbele yake. Lakini Mordekayi hakuinama wala kupiga magoti mbele yake.

3Wakubwa mbalimbali wa mufalme waliokuwa kwenye mulango wa mufalme, wakamwuliza Mordekayi: “Mbona wewe unaizarau amri ya mufalme?”

4Kila siku walimushauria aache tabia hiyo, lakini Mordekayi hakukubaliana nao. Alikataa kufanya hivyo akisema kwamba yeye ni Muyuda na kwa hiyo hawezi kuinama mbele ya Hamani. Basi, wakamujulisha Hamani kusudi waone kama ataivumilia tabia ya Mordekayi.

5Hamani akawaka hasira alipojua kwamba Mordekayi hainami wala kupiga magoti mbele yake.

6Tena alipogundua kwamba Mordekayi alikuwa Muyuda, akaamua kwamba kumwazibu peke yake haitoshi. Basi akafanya shauri la kuwaangamiza Wayuda wote, watu wa ukoo wa Mordekayi, katika utawala wa mufalme Ahasuero.

7Katika mwaka wa kumi na mbili wa utawala wa mufalme Ahasuero, katika mwezi wa kwanza unaoitwa Nisani, wakapiga Purimu, maana yake kura, mbele ya Hamani kusudi ajue mwezi na siku ya kuwaangamiza. Basi kura ikaangukia mwezi wa kumi na mbili unaoitwa Adari.

8Basi, Hamani akamwambia mufalme: “Kuna watu wa taifa moja wanaokuwa kila nafasi katika utawala wako, nao wako katika kila jimbo. Watu hao wana sheria zinazokuwa tofauti kabisa na za watu wengine. Vilevile, wao hawazitii sheria zako, kwa hiyo haikufaidii kwa kitu chochote kuwavumilia.

9“Ikikupendeza, ewe mufalme, amri itolewe, watu hawa waangamizwe. Nami ninaahidi, kama utaamuru hivyo, nitatoa kiasi cha kilo elfu kumi za feza iwekwe katika hazina ya mufalme.”

10Mufalme akaivua pete yake, ambayo ilitumiwa kwa kupiga muhuri juu ya matangazo, akamupa adui wa Wayuda Hamani mwana wa Hamedata wa uzao wa Agagi.

11Halafu mufalme akamwambia Hamani: “Umepewa watu wote na feza zile, tumia vile unavyopenda.”

12Basi, siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kwanza, Hamani akawaita waandishi wote wa mufalme, akawapa tangazo ambalo alitaka litafsiriwe kwa kila luga na kila namna ya maandiko katika utawala ule, na halafu mifano ya barua isambazwe kwa watawala wote, wakubwa wa majimbo yote, na viongozi wa makabila – kufuatana na luga zinazotumika kwao. Tangazo hilo likatolewa kwa jina la mufalme Ahasuero, na kupigwa muhuri kwa pete yake.

13Wajumbe wakazipeleka barua hizo kwa kila jimbo katika utawala ule. Tangazo hilo lilisema kwamba kwa siku moja tu, ni kusema siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili unaoitwa Adari, Wayuda wote – tangia kwa vijana mpaka wazee, wanawake na watoto, wote wauawe, waangamizwe na kuteketezwa kabisa, na mali zao zote zinyanganywe.

14Barua hiyo ilitakiwa iandikwe kwa watu wote katika kila jimbo, kusudi kila mutu ajitayarishe kwa ajili ya siku hiyo.

15Kwa amri ya mufalme, tangazo hili lilitolewa katika muji mukubwa wa Susani, nao wajumbe wakalitangaza katika majimbo yote. Mufalme na Hamani wakaikaa chini kwa kunywa wakati watu katika muji wa Susani wanafazaika.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help