2 Wafalme 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Elia ananyanyuliwa mbinguni

1Wakati ulifika ambapo Yawe alitaka kumupandisha Elia mbinguni katika upepo wa kuzungukazunguka. Elia na Elisha walikuwa katika njia, wakitoka Gilgali.

2Walipokuwa katika njia, Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Beteli.”

Lakini Elisha akamwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.”

Basi, wakaenda pamoja mpaka Beteli.

3Wanafunzi wa manabii wa Beteli wakamwendea Elisha, wakamwuliza: “Unajua kwamba leo Yawe atamupeleka bwana wako?”

Elisha akajibu: “Ndiyo. Ninajua. Munyamaze.”

4Kisha Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Yeriko.” Lakini Elisha akakataa akisema: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja mpaka Yeriko.

5Wanafunzi wa manabii wa Yeriko wakamwendea Elisha, wakamwuliza: “Unajua kwamba leo Yawe atamupeleka bwana wako?” Elisha akawajibu: “Ndiyo. Ninajua. Munyamaze.”

6Kisha Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Yordani.”

Lakini Elisha akasema: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja.

7Manabii makumi tano wakawafuata mpaka kwenye muto Yordani. Elia na Elisha wakasimama karibu na muto, nao manabii wakasimama mbali kidogo.

8Elia akavua nguo yake, akaikunja na kupiga nayo maji. Maji yakagawanyika katika sehemu mbili, nao wakavuka mpaka ngambo, wakipitia pahali pakavu.

9Walipofika ngambo, Elia akamwambia Elisha: “Uniambie jambo unalotaka nikufanyie mbele sijaondolewa kwako.”

Elisha akamwambia: “Ninaomba sehemu mara mbili ya roho yako.”

10Elia akajibu: “Ombi lako ni gumu. Hata hivyo, ikiwa utaniona wakati nitakapoondolewa kwako, itafanyika vile kwako. Lakini usiponiona, basi haitafanyika vile.”

11Walipokuwa wanatembea na kuongea, kwa rafla gari la moto lililokokotwa na farasi wa moto likawatenganisha. Naye Elia akanyanyuliwa mbinguni katika upepo wa kuzungukazunguka.

12Elisha alipoona tukio hilo, akalia: “Baba yangu, baba yangu! Ulikuwa wa lazima kuliko magari ya Israeli na wapanda-farasi wake!” Basi, Elisha hakumwona tena Elia.

Halafu Elisha akashika nguo zake na kuzipasua vipande viwili.

13Kisha akaokota nguo ya Elia iliyomwangukia, akarudia na kusimama kwenye ukingo wa muto Yordani.

14Akayapiga maji kwa nguo ya Elia akisema: “Yuko wapi Yawe, Mungu wa Elia?” Alipopiga maji, yakagawanyika sehemu mbili, naye akavuka mpaka ngambo.

15Wale wanafunzi wa manabii kutoka Yeriko walipomwona, walisema: “Roho wa Elia yuko kwa Elisha.” Basi, wakaenda kumupokea, wakainama mbele yake kwa heshima.

16Wakamwambia: “Sisi watumishi wako tuko na mashujaa makumi tano. Tafazali, uwaruhusu waende kumutafuta bwana wako. Labda roho wa Yawe amemubeba na kumutupa juu ya mulima fulani au katika bonde.”

Elisha akajibu: “Hapana, musiwatume.”

17Lakini wao walimwuzi sana mpaka akaona haya, akawaambia: “Muwatume.” Hivyo wakawatuma watu makumi tano, wakaenda wakamutafuta kila fasi kwa muda wa siku tatu nao hawakumwona.

18Kisha wakarudi kwa Elisha aliyekuwa anawangojea kule Yeriko. Elisha akawauliza: “Sikuwaambia musiende?”

Miujiza ya Elisha

19Kisha watu wa Yeriko wakamwendea Elisha, wakamwambia: “Bwana, kama vile unavyoona, muji huu ni muzuri, lakini maji tunayokuwa nayo ni mabaya na yanasababisha mimba kuharibika.”

20Elisha akawaambia: “Mutie chumvi ndani ya bakuli jipya, kisha muniletee.” Nao wakamuletea.

21Elisha akaenda kwenye chemichemi ya maji, akatupa chumvi hiyo ndani na kusema: “Yawe anasema hivi: Nimeyafanya maji haya kuwa yenye kufaa. Tangu sasa hayatasababisha vifo au kutoa mimba.”

22Na maji hayo yakakuwa ya kufaa mpaka leo, kama vile Elisha alivyosema.

23Elisha aliondoka Yeriko, akaenda Beteli. Alipokuwa katika njia, vijana wamoja walitoka katika muji, wakaanza kumuzomea wakisema: “Kwenda zako, kwenda zako muzee wa upaa!”

24Elisha aligeuka, akawaangalia na kuwalaani kwa jina la Yawe. Dubu wawili wakatoka katika pori, wakawararua vijana makumi ine na wawili kati yao.

25Elisha akaendelea na safari yake mpaka kwenye mulima Karmeli na tokea kule akarudi Samaria.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help