1Waisraeli wote pamoja wakalalamika na kulia usiku ule.
2Wakamunungunikia Musa na Haruni wakisema: Afazali tungekufia Misri! Afazali tungekufia hapahapa katika jangwa!
3Kwa nini Yawe anatupeleka katika inchi hiyo? Tutauawa katika vita, na wake zetu na watoto wetu watakamatwa mateka! Si afazali turudi Misri?
4Basi wakaanza kuambiana: Tuchague kiongozi, turudi Misri.
5Hapo, Musa na Haruni wakaanguka uso mpaka chini mbele yao.
6Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, ambao walikuwa kati ya wale watu waliokwenda kupeleleza hiyo inchi, wakararua nguo zao
7na kuwaambia Waisraeli: Inchi tuliyokwenda kupeleleza ni nzuri sana.
8Ikiwa Yawe amependezwa nasi, atatupeleka huko na kutupatia inchi inayotiririka maziwa na asali.
9Lakini musimwasi tu Yawe, wala musiwaogope wenyeji wa inchi hiyo. Maana wao ni kama mboga tu kwetu. Kingo yao imekwisha kuondolewa kwao naye Yawe yuko pamoja nasi. Musiwaogope! Ang. Ebr 3.16
10Lakini wengine wote pamoja wakatishia kuwapiga mawe. Kwa rafla, utukufu wa Yawe ukatokea juu ya hema la mukutano, mbele ya watu wote wa Israeli.
Musa anawaombea watu11Kisha Yawe akamwambia Musa: Watu hawa watanizarau mpaka wakati gani? Na mpaka wakati gani wataendelea kutoniamini, hata pamoja na vitambulisho vyote nilivyotenda kati yao?
12Nitawapiga kwa ugonjwa mukali na kuwatupilia mbali; lakini, kutokana nawe, nitaunda taifa lingine kubwa, lenye nguvu kuliko wao.
13Lakini Musa akamwambia Yawe: Uliwatoa watu hawa katika inchi ya Misri kwa nguvu yako. Wamisri watakaposikia kwamba umewatendea watu wako hivyo, Ang. Kut 32.11-14
14watawapasha wakaaji wa inchi habari hii. Maana watu hawa wamekwisha kupata habari kwamba wewe, ee Yawe, uko pamoja nasi; maana wewe, ee Yawe, unaonekana waziwazi wingu lako linaposimama juu yetu, na kwamba wewe unatutangulia muchana kwa nguzo ya wingu na usiku kwa nguzo ya moto.
15Sasa basi, ukiwaua watu wako wote kwa mara moja, mataifa ambayo yamekwisha kusikia sifa zako yatasema:
16Yawe aliwaua watu wake katika jangwa kwa sababu alishindwa kuwapeleka katika inchi aliyoahidi kuwapa.
17Basi, sasa ninakusihi, ee Yawe, utuonyeshe uwezo wako kwa kufanya kama ulivyotuahidi uliposema:
18“Mimi Yawe si mwepesi wa hasira, ni mwenye wema mwingi, na ni mwenye kusamehe uovu na makosa. Lakini kwa vyovyote vile sitakosa kuwaazibu watoto na wajukuu mpaka kizazi cha tatu na cha ine kwa zambi za wazazi wao.” Ang. Kut 20.5-6; 34.6-7; Kumb 5.9-10; 7.9-10
19Ninakusihi uwasamehe watu hawa zambi zao, kadiri ya wema wako mwingi kama vile ulivyowasamehe tangu watoke Misri mpaka sasa.
20Yawe akajibu: Nimewasamehe kama vile ulivyoomba.
21Lakini kwa kweli, kama vile ninavyoishi na kama vile dunia itakavyojaa utukufu wa Yawe, Ang. Ebr 3.18
22hakuna hata mumoja wao ambaye amekwisha kuuona utukufu wangu na vitambulisho vyangu nilivyofanya Misri na katika jangwa kisha akazidi kunijaribu mara hizi zote bila ya kutii sauti yangu,
23atakayeona inchi ile niliyoapa kuwapatia babu zao. Vilevile hata wale wanaonizarau hawataiona.
24Lakini kwa sababu mutumishi wangu Kalebu ni tofauti, na amenitii kwa ukamilifu, nitamufikisha kwenye inchi hiyo aliyoingia ndani yake na wazao wake watairizi. Ang. Yos 14.9-12
25Kwa sababu Waamaleki na Wakanana wanakaa katika mabonde ya inchi hiyo, kesho mugeuke nyuma muende katika jangwa kuelekea bahari ya Shamu.
26Kisha Yawe akamwuliza Musa na Haruni:
27Kundi hili la watu waovu litaendelea kuninungunikia mpaka wakati gani? Nimechoka na haya manunguniko ya Waisraeli juu yangu!
28Sasa uwajibu hivi: Yawe anasema hivi: Kama vile ninavyoishi, nitawatendea ninyi yaleyale niliyosikia mukiyasema:
29Mutakufa na miili yenu itatupwa humuhumu katika jangwa, kwa sababu mumenungunika juu yangu, hakuna hata mumoja wenu mwenye umri wa kuanzia miaka makumi mbili na zaidi, Ang. Ebr 3.17
30atakayeingia katika inchi hiyo ambayo niliapa kuwapa ikuwe yenu, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni.
31Ninyi mulisema kwamba watoto wenu watakamatwa mateka, lakini mimi nitawafikisha watoto wenu katika inchi muliyoizarau, kusudi waijue na ikuwe makao yao.
32Lakini ninyi, mutakufia humuhumu katika jangwa.
33Watoto wenu watatangatanga na kutaabika humu katika jangwa kwa muda wa miaka makumi ine kwa ajili ya ukosefu wenu wa imani mpaka mutu wenu wa mwisho atakapokufia katika jangwa.
34Kutokana na makosa yenu, mutataabika kwa muda wa miaka makumi ine, sawa na zile siku makumi ine mulizopeleleza ile inchi, mwaka mumoja kwa kila siku moja; mutatambua kwamba mimi nimechukizwa.
35Mimi Yawe nimesema: Hakika nitawatendea hivyo ninyi wote muliokusanyika hapa kwa kunipinga. Wote wataishia humuhumu katika jangwa na ni humu watakamokufia.
36Wale watu ambao Musa aliwatuma kwenda kupeleleza ile inchi waliorudi na kusababisha watu wamunungunikie Yawe kwa kuleta habari ya uongo juu ya inchi,
37watu hao waliotoa habari za uongo juu ya hiyo inchi, wakakufa kwa pigo mbele ya Yawe.
38Lakini Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, wakabaki wazima kati ya wale watu waliokwenda kupeleleza inchi.
Jaribio la kwanza la kushambulia inchi(Kumb 1.41-46)39Musa akawaambia Waisraeli wote nao wakalia kwa uchungu mwingi.
40Kesho yake, wakaamuka asubui mapema wakaenda sehemu za milima, wakisema: Sasa tuko tayari kabisa kwenda pahali ambapo Yawe alituahidi. Tunaitika kwamba tulitenda zambi.
41Lakini Musa akasema: Sasa mbona munavunja agizo la Yawe? Hivyo hamutashinda!
42Musiende kule kwenye milima kusudi musipigwe bure na waadui zenu, maana, Yawe hayuko pamoja nanyi.
43Mukiwashambulia Waamaleki na Wakanana, mutakufia katika vita kwa sababu mumeacha kumufuata Yawe. Yeye hatakuwa pamoja nanyi.
44Hata hivyo, wao wakakazana kwenda juu kwenye milima, ingawa Sanduku la Agano la Yawe, wala Musa hakuondoka katika kambi.
45Halafu Waamaleki na Wakanana, waliokuwa wakiishi katika inchi hiyo ya milima, wakashuka, wakawashambulia na kuwashinda. Wakawafukuza mpaka muji wa Horma.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.