Ufunuo 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Nyama wawili wa ajabu

1Kisha nikaona nyama mumoja wa ajabu akitokea ndani ya bahari. Alikuwa na vichwa saba na pembe kumi. Na juu ya kila pembe lake kulikuwa taji, na juu ya vichwa vile kulikuwa kumeandikwa jina la kumutukana Mungu.

2Yule nyama niliyemwona alifanana na chui. Miguu yake ilikuwa kama ya dubu na kinywa chake kilikuwa kama kinywa cha simba. Yule nyoka mukubwa akamupa uwezo wake pamoja na kiti chake cha kifalme na mamlaka makubwa.

3Kimoja cha vichwa vya yule nyama kilionekana kwamba kilikuwa kimeumizwa vibaya sana, lakini kidonda kilichokuwa cha hatari ya kufa kilikuwa kimekwisha kupona. Na kwa hiyo watu wote wa dunia wakashangaa na kumufuata yule nyama.

4Nao wakaanza kumwabudu yule nyoka kwa sababu alimupa yule nyama uwezo wake. Vilevile wakamwabudu yule nyama, wakisema: “Ni nani anayefanana na nyama huyu? Ni nani anayeweza kupigana vita naye?”

5Yule nyama akapewa uwezo wa kusema maneno ya kiburi ya kumutukana Mungu. Naye akapewa mamlaka ya kufanya kazi yake kwa muda wa miezi makumi ine na miwili.

6Basi yule nyama akaanza kumutukana Mungu, akatukana jina lake na makao yake na wale wanaokaa mbinguni.

7Akapewa ruhusa ya kupigana vita na watu wa Mungu na kuwashinda. Akapewa hata mamlaka ya kutawala watu wote, wa kila kabila, kila jamaa, kila luga na kila taifa.

8Wakaaji wote wa dunia watamwabudu, ndio wale wote ambao tangia kuumbwa kwa dunia, majina yao hayakuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo aliyechinjwa.

9“Mwenye kuwa na masikio, asikie.

10Mutu yule aliyekusudiwa kuwa mufungwa, atafungwa; na yule aliyekusudiwa kuuawa kwa upanga, atauawa kwa upanga. Kwa sababu hiyo, watu wa Mungu wanapaswa kuwa wavumilivu na wenye imani.”

11Kisha nikaona nyama wa pili wa ajabu akitokea ndani ya udongo. Alikuwa na pembe mbili zinazokuwa kama za mwana-kondoo naye alikuwa akisema kama nyoka mukubwa.

12Yeye alitumikisha mamlaka yote aliyopewa na yule nyama wa kwanza mbele yake. Alilazimisha vyote vinavyokuwa katika dunia pamoja na wakaaji wake kumwabudu yule nyama wa kwanza aliyekuwa na kovu la kidonda cha hatari.

13Yule nyama mukubwa wa pili alifanya kitambulisho kikubwa hata akashusha moto toka mbinguni mpaka juu ya dunia mbele ya watu wote.

14Akawadanganya wakaaji wa dunia kwa njia ya vitambulisho alivyowezeshwa kuonyesha mbele ya yule nyama mukubwa wa kwanza. Aliwaambia watu wa dunia watengeneze sanamu kwa heshima ya yule nyama aliyeumizwa kwa upanga, lakini aliendelea kuishi.

15Kisha yule nyama mukubwa wa pili akapewa uwezo wa kupuliza pumzi ya uzima ndani ya sanamu ya yule nyama mukubwa wa kwanza kusudi sanamu ile ipate kusema na kuweza kuua watu wasioiabudu.

16Na yule nyama akawalazimisha watu wote, wadogo na wakubwa, watajiri na wamasikini, wanaokuwa huru na watumwa, wapigwe chapa juu ya mikono yao ya kuume na juu ya paji za nyuso zao.

17Na hakukukuwa mutu aliyeweza kununua wala kuuzisha kitu pasipo kuwa na chapa ya jina la nyama yule au tarakimu zinazolingana na herufi za jina lile.

18Hapa inafaa kuwa na hekima. Yule anayekuwa na akili afafanue hesabu ya tarakimu zinazolingana na jina la yule nyama, kwa maana tarakimu ile ni ya mutu fulani. Nayo ni mia sita makumi sita na sita.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help