1 Samweli 28 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Nyuma ya muda fulani, Wafilistini walikusanya waaskari wao tayari kwenda kupigana na Waisraeli. Akisi akamwambia Daudi: “Uelewe vizuri kwamba wewe na watu wako munapaswa kwenda pamoja nami kupigana vita.”

2Daudi akamujibu Akisi: “Kweli! Utaona kitu ambacho mutumishi wako anaweza kufanya.”

Akisi akamwambia: “Nami nitakufanya kuwa mulinzi wangu wa pekee wa maisha.”

3Wakati ule, Samweli alikuwa amekwisha kufa, na Waisraeli wote walikuwa wamekwisha kumwombolezea na kumuzika katika muji wake Rama. Saulo alikuwa amewafukuza kutoka katika inchi wenye kutabiri na wachawi.

4Wafilistini walikusanyika na kupiga kambi yao kule Sunemi; na Saulo aliwakusanya Waisraeli wote na kupiga kambi yao kwenye mulima Gilboa.

5Saulo alipoona kundi la waaskari wa Wafilistini, alianza kuogopa, akaanza kutetemeka kwa hofu aliyokuwa nayo ndani ya moyo wake.

6Hata alipomwomba Yawe shauri, Yawe hakumujibu kwa ndoto, kwa mawe ya kupiga kura, wala kwa njia ya manabii.

7Halafu Saulo akawaambia watumishi wake: “Munitafutie mwanamuke ambaye anaweza kuaguza kusudi nimwendee na kumwomba shauri.” Watumishi wake wakamujibu: “Kuna mwanamuke mwaguzi mumoja kule Endori.”

8Basi, Saulo akajigeuza na kuvaa nguo zingine, akaenda kule pamoja na watu wake wawili. Walifika kwa yule mwanamuke usiku. Saulo akamwambia: “Unifanyie uaguzi na kunipandishia mutu yeyote nitakayekutajia.”

9Yule mwanamuke akamwambia: “Wewe unajua kwa hakika kwamba mufalme Saulo amewaangamiza kabisa waaguzi na wachawi wote katika inchi ya Israeli. Sasa kwa nini unaniwekea mutego wa kuninasa na kuniua?”

10Saulo akamwapia kwa jina la Yawe, akisema: “Kama vile Yawe anavyoishi, hakuna azabu yoyote itakayokupata kutokana na jambo hili.”

11Yule mwanamuke akamwuliza: “Nikupandishie nani kutoka kule?”

Saulo akajibu: “Unipandishie Samweli.”

12Yule mwanamuke alipomwona Samweli akalalamika kwa sauti kubwa, akamwambia Saulo: “Kwa nini umenidanganya? Wewe ni Saulo!”

13Mufalme Saulo akamwambia: “Usiogope! Unaona nini?”

Yule mwanamuke akamujibu: “Ninaona mungu akipanda toka ndani ya udongo.”

14Saulo akamwambia yule mwanamuke: “Ni mufano wa nani?”

Yule mwanamuke akamwambia: “Mwanaume muzee anapanda juu, naye anajifunika kanzu.” Halafu, Saulo akatambua kwamba yule ni Samweli. Saulo akainama uso mpaka chini, kwa heshima.

15Samweli akamwambia Saulo: “Kwa nini unanisumbua kwa kunipandisha?”

Saulo akamujibu: “Mimi nina taabu kubwa! Wafilistini wananishambulia kwa vita, na Mungu ameniachilia. Hanijibu tena kwa njia ya manabii wala kwa ndoto. Ndiyo maana nimekuita unijulishe kitu cha kufanya.”

16Samweli akasema: “Kwa nini unaniomba shauri ikiwa Yawe amekuachilia na amekuwa adui yako?

17Yawe amekutendea kile alichokuambia kwa njia yangu. Yawe ameurarua ufalme kutoka katika mikono yako, na amemupa Daudi jirani yako.

18Maana, wewe haukuitii sauti ya Yawe, wala haukuitimiza kasirani yake juu ya Waamaleki. Ndiyo maana leo Yawe amekutendea mambo haya.

19Zaidi ya hayo, Yawe atakutia wewe pamoja na Waisraeli wote katika mikono ya Wafilistini. Kesho, wewe na wana wako mutakuwa pamoja nami. Hata waaskari wa Israeli, Yawe atawatia katika mikono ya Wafilistini.”

20Kwa rafla, Saulo akiwa na hofu kutokana na maneno ya Samweli, alianguka chini. Hakukuwa na nguvu zozote kwa sababu alikuwa hajakula kitu chochote kwa siku nzima, usiku na muchana.

21Halafu yule mwanamuke alimwendea Saulo, na alipoona kwamba Saulo ameshikwa na hofu sana, alimwambia: “Mimi mutumishi wako nimehatarisha maisha yangu kwa kufanya kile ulichoniambia nikufanyie.

22Sasa, unisikilize mimi mutumishi wako. Nitakutayarishia mukate kusudi ukule nawe utakuwa na nguvu za kuendelea na safari yako.”

23Lakini Saulo alikataa na kusema: “Sitakula.”

Lakini watumishi pamoja na yule mwanamuke, walimusihi akule, naye akawasikiliza. Kwa hiyo alisimama kutoka chini na kuikaa kwenye kitanda.

24Yule mwanamuke alikuwa na mwana-ngombe wake mumoja katika nyumba yake aliyenona, akamuchinja haraka, akatwaa unga wa ngano, akauponda, akatengeneza mukate usiotiwa chachu.

25Akamupa Saulo, akawapa vilevile watumishi wake, nao wakakula. Halafu wakaondoka na kwenda zao wakati uleule wa usiku.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help