1 Wakorinto 14 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maneno mapya juu ya zawadi ya Roho Mutakatifu

1Mujikaze mukuwe na upendo. Vilevile mutamani sana kupata zawadi za Roho, hasa zaidi zawadi ya kutabiri.

2Mutu anayesema kwa luga ya ajabu hasemi na watu lakini anasema na Mungu, kwa maana hakuna mutu anayemusikia. Kwa uwezo wa Roho, mutu yule anasema mafumbo.

3Lakini yule anayetabiri anasema na watu maneno ya kuwajenga katika imani, kuwatia moyo na kuwatuliza.

4Yule anayesema kwa luga ya ajabu anajenga imani yake mwenyewe, lakini yule anayetabiri anajenga imani ya kanisa zima.

5Ninataka ninyi wote museme kwa luga za ajabu, lakini ninataka zaidi tena mupate kutabiri. Kwa maana, yule anayetabiri ni wa lazima kuliko yule anayesema kwa luga za ajabu, isipokuwa kama huyo mutu anaweza kutafsiri yale anayosema kusudi kanisa zima lijengwe katika imani.

6Basi wandugu zangu, nitawafalia nini kama nikikuja kwenu na kusema nanyi katika luga za ajabu? Sitawafalia kitu pasipo kuwaelezea maneno ya ufunuo, au ya elimu, pasipo kuwatabiria au kuwafundisha.

7Tuangalie mufano wa vyombo vya muziki kama vile filimbi au kinanda. Milio ya vyombo hivi isipokuwa mbalimbali, namna gani mutu anavyoweza kutambua wimbo unaopigwa?

8Ngunga isipopigwa kwa mulio wa kuarifu, askari gani atakayeweza kujitayarisha kwa vita?

9Ni hivi vilevile mambo munayosema yatatambulikana namna gani ikiwa maneno munayoeleza kwa luga za ajabu hayako wazi? Kwa maana mutakuwa kama wenye kusema na upepo.

10Kuna namna mbalimbali za luga katika dunia, lakini hakuna hata moja isiyokuwa na maana.

11Basi kama nisipojua luga fulani, nitakuwa kama mujinga kwa yule anayeisema, naye atakuwa kama mujinga kwangu.

12Hivi vilevile kufuatana na vile munavyotamani sana zawadi za Roho, mujikaze kupata kwa uwingi zile zinazoweza kujenga kanisa katika imani.

13Kwa hiyo yule anayesema kwa luga ya ajabu, aombe Mungu amupatie uwezo wa kuitafsiri.

14Kwa maana kama nikiomba katika luga ya ajabu, roho yangu inaomba, lakini akili yangu haitumiki.

15Basi ninapaswa kufanya nini? Nitaomba katika roho na katika akili vilevile. Nitaimba katika roho na katika akili vilevile.

16Kwa maana kama ukimwomba Mungu ndani ya roho tu kwa kumushukuru, mutu asiyeelewa kitu anayehuzuria katika mukutano hawezi kusema amina kwa kuitikia maombi yako ya kushukuru. Ni kwa sababu hasikii mambo unayosema.

17Ijapokuwa ni kweli maombi yako ya kushukuru yanawezekana kuwa mazuri, lakini hayajengi mutu mwingine katika imani.

18Ndiyo, ninamushukuru Mungu kwamba ninasema kwa luga za ajabu kuliko ninyi wote.

19Lakini, katika mukutano ninapenda kusema maneno matano yenye kusikilika, kusudi niwafundishe wengine, kuliko kusema maneno elfu kumi kwa luga za ajabu.

20Wandugu zangu, musikuwe kama watoto kwa kufikiri: lakini katika mambo mabaya, iwatokee kutenda kama watoto wachanga. Inafaa mafikiri yenu yakuwe kama ya watu wazima.

21Imeandikwa katika Sheria:

“Bwana anasema:

‘Nitasema na watu hawa

kwa njia ya wageni wenye luga ngeni

Na hata hivi hawatanisikiliza.’ ”

22Kwa hiyo, zawadi ya kusema luga za ajabu ni kitambulisho kwa wasioamini, lakini si kwa waamini. Na zawadi ya kutabiri ni kitambulisho kwa waamini, lakini si kwa wasioamini.

23Basi kama kanisa zima limekusanyika, na watu wote wanaanza kusema kwa luga za ajabu; na kisha watu wasioelewa kitu au wasioamini wakiingia katika mukutano wenu hawatasema kuwa ninyi ni wenda-wazimu?

24Lakini kama wote wakitabiri, na kama mutu mumoja asiyeamini au asiyeelewa kitu anaingia, atapata uhakikisho kutokana na maneno ya hao wote. Naye atahukumiwa kufuatana na yote aliyosikia na

25kufichuliwa waziwazi mawazo yake aliyoficha. Na hivi atainama uso mpaka chini na kumwabudu Mungu, akisema: “Kweli Mungu ni katikati yenu!”

Utaratibu katika kanisa

26Wandugu zangu, niseme nini basi? Wakati munapokusanyika kwa ibada, mumoja anaweza kuimba wimbo, mwingine kufundisha, mwingine kutoa ufunuo, mwingine kusema kwa luga za ajabu na mwingine anaweza kutafsiri. Na hayo yote yanapaswa kufanyika katika nia ya kujenga kanisa katika imani.

27Kukiwa wenye kusema kwa luga za ajabu, inafaa wasikuwe zaidi ya wawili au watatu, nao waseme mumoja kwa mumoja. Na tena kunapaswa kuwa mutu wa kutafsiri maneno wanayosema.

28Kama hakuna mutu anayetafsiri, basi kila mumoja wao anyamaze katika mukutano, aseme tu ndani ya moyo, yeye mwenyewe na Mungu.

29Na kwa upande wa wale wanaotabiri, wanaweza kusema wawili au watatu na watu wengine wapime yale wanayosema.

30Lakini kukiwa mutu anayesema, na mwingine anayekaa karibu akipata ufunuo, inafaa yule anayesema anyamaze.

31Kwa maana ninyi wote munaweza kutabiri mumoja kwa mumoja, kusudi wote wapate kufundishwa na kutiwa moyo.

32Zawadi ya unabii inapaswa kuwa chini ya utawala wa yule aliyeipewa,

33kwa maana Mungu hataki sisi tuishi katika fujo, lakini katika amani. Sawa vile inavyokuwa desturi katika makanisa yote ya watu wa Mungu,

34wanawake wanapaswa kukaa kimya katika mikutano ya kanisa. Wao hawaruhusiwi kusema katika kanisa, lakini wanapaswa kutii sawa vile Sheria inavyosema.

35Kama wakiwa na neno la kuuliza, waulize waume wao kwenye nyumba zao. Ni haya kwa mwanamuke kusema katika mukutano wa kanisa.

36Munazani kwamba Neno la Mungu limetoka kwenu au limewafikia ninyi peke yenu tu?

37Kama mutu akizani kwamba yuko na zawadi ya unabii au zawadi ingine ya Roho, anapaswa kujua kwamba maneno haya ninayowaandikia ninyi ni amri ya Bwana.

38Lakini kama yeye hajui vile, basi mutu asishugulike naye.

39Kwa hiyo wandugu zangu, mutamani sana kupata zawadi ya kutabiri, nanyi musiwazuize watu kusema kwa luga za ajabu.

40Lakini maneno yote yatendeke katika usawa na katika utaratibu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help