Mika 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Malalamiko ya nabii

1Ole wangu!

Mimi ninakuwa kama muvunaji kisha wakati wa mavuno;

hakuna tini za kwanzakwanza ninazotamani.

Ni kama wakati wa kuchuma zabibu:

hakuna hata fungu moja la zabibu la kula!

2Hakuna mutu mwaminifu kwa Mungu aliyebaki katika inchi,

hakuna mutu yeyote mwenye usawa kati ya watu.

Kila mumoja anavizia kumwanga damu;

kila mumoja anamwinda mwenzake kusudi amunase.

3Wote ni wafundi wa kutenda maovu;

waongozi na waamuzi wanaomba kituliro.

Wakubwa wanaonyesha wazi nia zao mbaya,

nao wanashirikiana pamoja kwa kuzitimiza.

4Mutu muzuri zaidi kati yao ni kama michongoma,

naye mwenye usawa zaidi ni hatari kama upango wa miiba.

Siku iliyongojewa ya azabu yao imefika.

Na sasa mahangaiko yamewapata.

5Usimwaminie mwenzako,

wala usimutumainie rafiki yako.

Chunga mudomo wako,

usimwambie kitu muke wako wewe mwenyewe.

6Maana, mutoto mwanaume anamuzarau baba yake;

mutoto mwanamuke anabishana na mama yake,

muke wa mwana anapingana na mama mukwe wake.

Waadui wa mutu ni watu wa nyumba yake.

7Lakini mimi ninamutumainia Yawe,

ninamutazamia Mungu mwenye kuniokoa;

Mungu wangu atanisikiliza.

Tumaini na maombi ya watu

8Usifurahie hali yangu ewe adui yangu!

Nikianguka, nitasimama tena;

nikiwa katika giza, Yawe ni mwangaza wangu.

9Kwa vile nimemukosea Yawe,

nitavumilia kasirani yake,

mpaka atakapotetea maneno yangu

na kunijalia haki yangu.

Atanileta inje kwenye mwangaza,

nami nitaona akisimamisha haki.

10Halafu adui yangu ataona hayo

naye atafunikwa na haya;

maana aliniambia: Basi Yawe, Mungu wako, yuko wapi?

Mimi mwenyewe nitamwona adui akianguka;

atakanyagwakanyagwa chini kama matope katika njia.

11Siku inakuja ambapo kuta za muji wenu zitajengwa upya.

Siku hiyo mipaka ya inchi yenu itapanuliwa.

12Siku hiyo wandugu zenu watawarudilia,

kutoka Asuria na vijiji vya Misri,

kutoka inchi ya Misri na eneo la muto Furati;

kutoka sehemu za maji na sehemu za milima.

13Lakini inchi yote nyingine itakuwa jangwa,

kwa sababu ya uovu wa wakaaji wake.

Maombi

14Ee Mungu, uwachunge watu wako kwa fimbo yako,

uwachunge wale wanaokuwa kundi lako mwenyewe

ambao wanaishi peke yao katika pori

na kuzungukwa na inchi yenye mboleo.

Uwachunge kama ulivyofanya pale zamani

katika shamba la malisho ya Basani na Gileadi.

15Kama wakati ulipotutoa toka katika inchi ya Misri,

utuonyeshe tena maajabu yako.

16Nao watu wa mataifa watakapoona hayo,

watafezeheka hata kama wana nguvu.

Watapigwa na bumbuazi na kukosa cha kusema

na kuwa kama viziwi.

17Watatambaa katika mavumbi kama nyoka,

kama viumbe vinavyotambaa.

Watatoka katika makimbilio yao

wakitetemeka na kujaa hofu.

Watakugeukia Yawe, Mungu wetu, kwa hofu,

wataogopa kwa sababu yako.

18Ee Mungu, ni nani anayekuwa kama wewe?

Wewe unasemehe zambi za watu wako waliobaki,

wala hauyaangalii makosa yao.

Hasira yako haidumu milele,

lakini unapendelea zaidi kutuonyesha wema wako.

19Utatuhurumia tena;

utatupilia mbali zambi zetu,

utazitupa zote katika vilindi vya bahari.

20Utatuonyesha uaminifu na wema wako

sisi wazao wa Abrahamu na wa Yakobo,

kama ulivyowaahidi babu zetu tangu zamani.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help