Yesaya 21 - Swahili Roehl Bible 1937

Kuangamia kwa Babeli.Tamko zito la kuwaambia wakaao nyikani kwenye bahari:

1Kama upepo wenye nguvu unavyovuma upande wa kusini,

ndivyo, mambo yanavyotoka nyikani katika nchi inayoogopwa.

2Nimefumbuliwa na kuonyeshwa yenye ugumu:

mdanganyifu hudanganya, naye mwangamizaji huangamiza.

Pandeni, Waelamu! Shambulieni, Wamedi!

Hivyo nitawanyamazisha wote waliowapigia kite.

3Kwa hiyo viuno vyangu vimeenea kukauka,

uchungu ukanishika kama uchungu wa mwanamke azaaye,

kizunguzungu kikanipata, nisisikie, nikastushwa, nisione.

4Roho yangu ikazimia, mastuko yakanigundua;

saa za jioni, nilizozipenda, zikawa za kunitetemesha.

5Wao hutandika meza, huweka wangoja zamu, hula, hunywa.

Mara wanaambiwa: Inukeni, wakuu! Zipakeni ngao mafuta!

6Kwani ndivyo, Bwana alivyoniambia:

Nenda, uweke mlinzi, akuambie, atakayoyaona!

7Atakapoona kikosi cha watu waliopanda farasi,

wakienda wawiliwawili,

hata kikosi cha punda na kikosi cha ngamia,

na aangalie sana kwa uangalifu mwingi.

8Akaita na kupaza sauti kama simba kwamba:

Bwana, hapa kilindoni mimi ninasimama mchana kutwa,

nao usiku kucha nimewekwa mimi kungoja hapa kidunguni.

9Sasa tazameni! Panakuja kikosi cha watu

waliopanda farasi wakienda wawiliwawili!

Kisha akasema: Umeanguka! Umeanguka mji wa Babeli!

Navyo vinyago vyake vyote vya miungu yao

amevivunja na kuvitupa chini.

10Ninyi wenzangu mliopigwa,

kama mpunga unavyopigwa penye kuupuria,

niliyoyasikia kwa Bwana Mwenye vikosi, Mungu wa Isiraeli,

nimewatangazia ninyi.

Patilizo la Edomu.

Tamko zito la kuwaambia Waduma:

11Toka Seiri wananiita kwamba:

Mlinzi, saa ngapi sasa za usiku?

Mlinzi, saa ngapi sasa za usiku?

12Mlinzi akajibu: Ijapo mapema yaje,

usiku utakuwa ungalipo.

Kama mnataka kuuliza mengine, haya! Ulizeni!

Patilizo la Arabia.

Tamko zito la kuwaambia Waarabu:

13Sharti mlale kwenye mapori nyikani,

ninyi watembezi wa Dedani!

14Waliokufa kiu wapelekeeni maji,

ninyi mkaao katika nchi ya Tema!

Waliokimbia wagawieni vilaji vya kuwatunza!

15Kwani wamezikimbia panga,

zile panga walizochomolewa wao,

wamezikimbia nazo pindi, walizovutiwa,

hata uzito wote wa vita.

16Kwani ndivyo, Bwana alivyoniambia:

Ungaliko bado mwaka, kama miaka ya kibarua ilivyo,

ndipo, utukufu wote wa Kedari utakapokuwa umekwisha.

17Watakaosalia kwa wana wa Kedari walio wenye nguvu

katika hesabu yao ya wavuta pindi watakuwa wachache,

kwani Bwana Mungu wa Isiraeli amevisema.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help