Yoshua Mwana wa Sira 13 - Bible in Kiswahili, Revised Union Version 2013

Tahadhari kuhusu Ushirikiano

1Mwenye kugusa lami atatiwa uchafu; naye mwenye kufuatana na mwenye kiburi atapata kufanana naye.

2Usijitwike mzigo upitao nguvu zako; wala usishirikiane na mtu aliye tajiri kuliko wewe. Jinsi gani chungu kushirikiana na birika? Hiyo itagonga na hicho kitavunjwa.

3Tajiri hudhulumu, akaogofya; maskini hudhulumiwa, akasihi.

4Iwapo una faida kwake, tajiri atachuma kwako; ukihitaji atakuacha.

5Kama una kitu, atakaa nawe; hata utakapofilisika, hajuti.

6Je! Ana haja nawe? Basi atakudanganya, na kukushawishi, na kukutia tumaini; atakupa maneno mazuri na kusema, Unahitaji nini?

7Naye atakutahayarisha kwa karamu zake; hata amekukumbia yote mara mbili tatu. Mwishowe atakufanyizia mzaha; atakuahirisha, na kukuacha, na kutikisa kichwa chake.

8Ujihadhari usije ukadanganyika na kufedheheshwa katika uchangamfu wako.

9Mkuu akikualika na uwe makini, hivyo atazidi kukualika.

10Usijitangulize kwake, usije ukakatazwa; wala usijitenge naye, usije ukasahauliwa.

11Usifanye kusema naye kama na mwenzako; wala usisadiki maneno yake mengi; yaani, kwa maongezi mengi atakujaribu, na kwa kukunjua uso atakupeleleza.

12Mtu asiyeficha moyoni mwake yaliyosemwa hana rehema; maana hatajizuia na kuhizi wala na kufunga;

13basi ujihadhari uwe macho, maadamu unakwenda katikati ya hatari ya kuanguka.

14-15Kila kiumbe hupenda kilichofanana nacho, na kila mwanadamu humpenda aliyefanana naye.

16Wanyama wote huandamana aina kwa aina; vile vile mwanadamu ataambatana na mmojawapo wa aina yake.

17Jinsi gani mbwamwitu ashirikiane na mwana-kondoo? Vivyo hivyo mwenye dhambi na mwenye haki.

18Kuna amani gani kati ya fisi na mbwa? Tena amani gani kati ya tajiri na maskini?

19Punda mwitu ni mawindo ya simba nyikani; ndivyo maskini walivyo malisho ya tajiri.

20Unyonge ni chukizo kwa mwenye kiburi; na umaskini ni chukizo kwa tajiri.

21Tena tajiri akitikisika huegemezwa na rafiki zake; mnyonge akiisha kuanguka husukumizwa mbali na rafiki zake.

22Tajiri akianguka, wapo wasidizi wengi; hata akinena yasiyoneneka, watu humkiri kuwa ana haki; mnyonge huanguka, na watu humshutumu; hata akitoa maneno ya hekima hakuna ampishaye.

23Tajiri anena, na wote wanyamaza na yale ayanenayo huyasifu hata mawinguni; maskini anena, nao husema, Nani huyu? Na iwapo amejikwaa, kumbe! Watazidi kumwangusha.

24Lakini utajiri pasipo dhambi ni mwema; na umaskini ni mbaya ukitoka katika ubaya.

25Moyo wa mtu hufanya kubadili uso,

Kwamba ni kwa wema au kwa ubaya.

26Uso mkunjufu hufunua moyo ulio fani;

Na kubuni mifano ni kuchosha akili.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help