Sefania 1 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

1Neno la Mwenyezi Mungu lililomjia Sefania mwana wa Kushi, mwana wa Gedalia, mwana wa Amaria, mwana wa Hezekia, wakati wa utawala wa Yosia mwana wa Amoni mfalme wa Yuda:

Onyo la maangamizi yanayokuja

2Mwenyezi Mungu asema,

“Nitafagia kila kitu

kutoka uso wa dunia.

3Nitafagilia mbali watu na wanyama;

nitafagilia mbali ndege wa angani

na samaki wa baharini.

Wafanyao maovu watapata tu kokoto,

nami nitamkatilia mbali mwanadamu atoke katika dunia,”

asema Mwenyezi Mungu.

Dhidi ya Yuda

4“Nitaiadhibu Yuda

na wote wanaoishi Yerusalemu.

Kutoka mahali hapa nitakatilia mbali

kila mabaki ya Baali,

majina ya wapagani na makuhani

waabuduo sanamu:

5wale ambao husujudu juu ya mapaa

kuabudu jeshi la vitu vya angani,

wale ambao husujudu na kuapa kwa Mwenyezi Mungu

na ambao pia huapa kwa Malkamu,

6wale wanaoacha kumfuata Mwenyezi Mungu,

wala hawamtafuti Mwenyezi Mungu

wala kutaka shauri lake.

7Nyamazeni mbele za Bwana Mungu Mwenyezi,

kwa maana siku ya Mwenyezi Mungu iko karibu.

Mwenyezi Mungu ameandaa dhabihu,

amewaweka wakfu wale aliowaalika.

8Katika siku ya dhabihu ya Mwenyezi Mungu

nitawaadhibu wakuu

na wana wa mfalme

na wale wote wanaovaa

nguo za kigeni.

9Katika siku hiyo nitaadhibu wote ambao

hukwepa kukanyaga kizingiti,

ambao hujaza hekalu la miungu yao

kwa dhuluma na udanganyifu.”

10Mwenyezi Mungu asema, “Katika siku hiyo

kilio kitapanda juu kutoka lango la Samaki,

maombolezo kutoka mtaa wa pili,

na mshindo mkubwa kutoka vilimani.

11Ombolezeni, ninyi mnaoishi katika eneo la sokoni;

wafanyabiashara wenu wote wameangamizwa,

wote ambao wanafanya biashara ya fedha

wataangamizwa.

12Wakati huo nitaupekua mji wa Yerusalemu kwa taa,

na kuwaadhibu wale ambao

wanakaa katika hali ya kuridhika,

ambao ni kama divai

iliyobaki kwenye machicha,

ambao hudhani, ‘Mwenyezi Mungu hatafanya lolote,

jema au baya.’

13Utajiri wao utatekwa nyara,

nyumba zao zitabomolewa.

Watajenga nyumba,

lakini hawataishi ndani yake;

watapanda mizabibu

lakini hawatakunywa divai yake.

Siku kubwa ya Mwenyezi Mungu

14“Siku kubwa ya Mwenyezi Mungu iko karibu:

iko karibu na inakuja haraka.

Sikilizeni! Kilio katika siku ya Mwenyezi Mungu

kitakuwa chungu.

Shujaa atapiga ukelele wa vita huko.

15Siku ile ni siku ya ghadhabu,

siku ya fadhaa na dhiki,

siku ya uharibifu na ukiwa,

siku ya giza na utusitusi,

siku ya mawingu na giza nene,

16siku ya tarumbeta na kelele za vita

dhidi ya miji yenye ngome,

na dhidi ya minara mirefu.

17Nitawaletea watu dhiki,

nao watatembea kama vipofu,

kwa sababu wametenda dhambi

dhidi ya Mwenyezi Mungu.

Damu yao itamwagwa kama vumbi

na matumbo yao kama kinyesi.

18Fedha yao wala dhahabu yao

hazitaweza kuwaokoa

katika siku hiyo ya ghadhabu ya Mwenyezi Mungu.

Katika moto wa wivu wake

dunia yote itateketezwa,

kwa maana ghafula ataleta mwisho

wa wote wanaoishi duniani.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help