Zaburi 111 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 111Sifa za Mwenyezi Mungu kwa matendo ya ajabu

1Msifuni Mwenyezi Mungu.

Nitamtukuza Mwenyezi Mungu kwa moyo wangu wote,

katika baraza la wanyofu na katika kusanyiko.

2Kazi za Mwenyezi Mungu ni kuu,

wote wanaopendezwa nazo huzitafakari.

3Kazi zake zimejaa fahari na utukufu,

haki yake hudumu daima.

4Amefanya maajabu yake yakumbukwe,

Mwenyezi Mungu ni mwenye neema na huruma.

5Huwapa chakula wale wanaomcha,

hulikumbuka agano lake milele.

6Amewaonesha watu wake uwezo wa kazi zake,

akiwapa nchi za mataifa mengine.

7Kazi za mikono yake ni za uaminifu na haki,

mausia yake yote ni ya kuaminika.

8Zinadumu milele na milele,

zikifanyika kwa uaminifu na unyofu.

9Aliwapa watu wake ukombozi,

aliamuru agano lake milele:

jina lake ni takatifu na la kuogopwa.

10Kumcha Mwenyezi Mungu ndicho chanzo cha hekima,

wote wanaozifuata amri zake wana busara.

Sifa zake zadumu milele.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help