Zaburi 51 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 51Kuomba msamahaKwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Baada ya kukemewa na nabii Nathani kwa kuzini na Bathsheba.

1Ee Mungu, unihurumie,

kwa kadiri ya upendo wako usiokoma,

kwa kadiri ya huruma yako kuu,

uyafute makosa yangu.

2Unioshe na uovu wangu wote

na unitakase dhambi yangu.

3Kwa maana najua makosa yangu,

na dhambi yangu iko mbele yangu daima.

4Dhidi yako, wewe peke yako, nimetenda dhambi

na kufanya yaliyo mabaya machoni pako,

ili uthibitike kuwa wa kweli unaponena,

na kuwa na haki unapotoa hukumu.

5Hakika mimi nilizaliwa mwenye dhambi,

mwenye dhambi tangu nilipotungwa mimba kwa mama yangu.

6Hakika wewe wapendezwa na kweli inayotoka moyoni;

wanifundisha hekima ndani ya moyo wangu.

7Nioshe kwa hisopo, nami nitakuwa safi,

unisafishe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji.

8Unipe kusikia furaha na shangwe,

mifupa uliyoiponda na ifurahi.

9Ufiche uso wako usizitazame dhambi zangu,

na uufute uovu wangu wote.

10Ee Mungu, uniumbie moyo safi,

uifanye upya roho ya uthabiti ndani yangu.

11Usinitupe kutoka mbele zako

wala kuniondolea Roho wako Mtakatifu.

12Unirudishie furaha ya wokovu wako,

unipe roho ya utii, ili initegemeze.

13Ndipo nitakapowafundisha wakosaji njia zako,

na wenye dhambi watarejea kwako.

14Ee Mungu, Mungu uniokoaye,

niokoe na hatia ya kumwaga damu,

nao ulimi wangu utaimba juu ya haki yako.

15Ee Bwana, fungua midomo yangu,

na kinywa changu kitatangaza sifa zako.

16Wewe hupendezwi na dhabihu, au ningeileta;

hufurahii sadaka za kuteketezwa.

17Bali dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika;

moyo uliovunjika wenye toba,

ee Mungu, hutaudharau.

18Kwa wema wa radhi yako uifanye Sayuni istawi,

ukazijenge upya kuta za Yerusalemu.

19Hapo ndipo kutakapokuwa na dhabihu za haki,

sadaka nzima za kuteketezwa za kukupendeza sana,

pia mafahali watatolewa

madhabahuni mwako.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help