Isaya 61 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Mwaka wa upendeleo wa Mwenyezi Mungu

1Roho wa Bwana Mungu Mwenyezi yu juu yangu,

kwa sababu Mwenyezi Mungu amenipaka mafuta

kuwahubiria maskini habari njema.

Amenituma kuwafariji waliovunjika moyo,

kuwatangazia mateka uhuru wao,

na hao waliofungwa

habari za kufunguliwa kwao;

2kutangaza mwaka wa Mwenyezi Mungu uliokubaliwa,

na siku ya kisasi ya Mungu wetu,

kuwafariji wote wanaoomboleza,

3na kuwapa mahitaji

wale wanaohuzunika katika Sayuni,

ili kuwapa taji za uzuri badala ya majivu,

mafuta ya furaha badala ya maombolezo,

vazi la sifa badala ya roho ya kukata tamaa.

Nao wataitwa mialoni ya haki,

pando la Mwenyezi Mungu,

ili kuonesha utukufu wake.

4Watajenga upya magofu ya zamani

na kupatengeneza mahali palipoachwa ukiwa zamani;

watafanya upya miji iliyoharibiwa,

iliyoachwa ukiwa kwa vizazi vingi.

5Wageni watayachunga makundi yenu,

wageni watafanya kazi katika mashamba yenu,

na kutunza mashamba yenu ya mizabibu.

6Nanyi mtaitwa makuhani wa Mwenyezi Mungu,

mtaitwa watumishi wa Mungu wetu.

Mtakula utajiri wa mataifa,

nanyi katika utajiri wao mtajisifu.

7Badala ya aibu yao

watu wangu watapokea sehemu maradufu,

na badala ya fedheha

watafurahia katika urithi wao;

hivyo watarithi sehemu maradufu katika nchi yao,

nayo furaha ya milele itakuwa yao.

8“Kwa maana Mimi, Mwenyezi Mungu, napenda haki,

na ninachukia unyang’anyi na uovu.

Katika uaminifu wangu nitawapa malipo yao

na kufanya agano la milele nao.

9Wazao wao watajulikana miongoni mwa mataifa,

na uzao wao miongoni mwa makabila ya watu.

Wale wote watakaowaona watatambua

kuwa ni taifa ambalo Mwenyezi Mungu amelibariki.”

10Ninafurahia sana katika Mwenyezi Mungu,

nafsi yangu inashangilia katika Mungu wangu.

Kwa maana amenivika mavazi ya wokovu,

na kunipamba kwa joho la haki,

kama vile bwana arusi apambavyo

kichwa chake kama kuhani,

na kama bibi arusi ajipambavyo

kwa vito vyake vya thamani.

11Kwa maana kama vile ardhi ifanyavyo chipukizi kuota,

na bustani isababishavyo mbegu kuota,

ndivyo Bwana Mungu Mwenyezi atafanya haki na sifa

zichipuke mbele ya mataifa yote.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help