Wimbo 1 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

1Wimbo ulio bora wa Sulemani.

Mpendwa

2Unibusu kwa busu la kinywa chako,

kwa maana upendo wako unafurahisha kuliko divai.

3Manukato yako yananukia vizuri,

jina lako ni kama manukato yaliyomiminwa.

Ndiyo sababu wanawali wanakupenda!

4Nichukue twende nawe, na tufanye haraka!

Mfalme na anilete ndani ya vyumba vyake.

Rafiki

Tunakushangilia na kukufurahia,

tutasifu upendo wako kuliko divai.

Mpendwa

Tazama jinsi ilivyo bora wakupende!

5Mimi ni mweusi, lakini napendeza,

enyi binti za Yerusalemu,

mweusi kama mahema ya Kedari,

kama mapazia ya hema la Sulemani.

6Usinikazie macho kwa sababu mimi ni mweusi,

kwa sababu nimefanywa mweusi na jua.

Wana wa mama yangu walinikasirikia

na kunifanya niwe mtunza mashamba ya mizabibu.

Shamba langu mwenyewe la mizabibu nimeliacha.

7Niambie, wewe ninayekupenda,

unalisha wapi kundi lako la kondoo

na ni wapi unapowapumzisha kondoo wako adhuhuri.

Kwa nini niwe kama mwanamke aliyefunikwa shela

karibu na makundi ya rafiki zako?

Rafiki

8Kama hujui, ewe mwanamke mzuri kuliko wote,

fuata nyayo za kondoo,

na kulisha wana-mbuzi wako

karibu na mahema ya wachungaji.

Mpenzi

9Mpendwa wangu, ninakufananisha na farasi jike

aliyefungwa katika mojawapo ya magari ya vita ya Farao.

10Mashavu yako yanapendeza yakiwa na vipuli,

shingo yako ikiwa na mikufu ya vito.

11Tutakufanyia vipuli vya dhahabu,

vyenye kupambwa kwa fedha.

Mpendwa

12Mfalme alipokuwa mezani pake,

manukato yangu yalisambaza harufu yake nzuri.

13Mpenzi wangu kwangu mimi ni kifuko cha manemane

kati ya matiti yangu.

14Mpenzi wangu kwangu mimi ni kama kishada cha maua ya mhina

kutoka mashamba ya mizabibu ya En-Gedi.

Mpenzi

15Tazama jinsi ulivyo mzuri, mpendwa wangu!

Tazama jinsi ulivyo mzuri!

Macho yako ni kama ya hua.

Mpendwa

16Tazama jinsi ulivyo mzuri, mpenzi wangu!

Ee, tazama jinsi unavyopendeza!

Na kitanda chetu ni cha majani mazuri.

Mpenzi

17Nguzo za nyumba yetu ni mierezi,

na mapao yetu ni miberoshi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help