Zaburi 143 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 143Maombi ya kuokolewa dhidi ya aduiZaburi ya Daudi.

1Ee Mwenyezi Mungu, sikia sala yangu,

sikiliza kilio changu unihurumie;

katika uaminifu na haki yako

njoo unisaidie.

2Usimhukumu mtumishi wako,

kwa kuwa hakuna mtu aliye hai

mwenye haki mbele zako.

3Adui hunifuatilia,

hunipondaponda chini;

hunifanya niishi gizani

kama wale waliokufa zamani.

4Kwa hiyo roho yangu inazimia ndani yangu,

moyo wangu ndani yangu unakata tamaa.

5Nakumbuka siku za zamani;

natafakari juu ya kazi zako zote,

naangalia juu ya kazi

ambazo mikono yako imezifanya.

6Nanyoosha mikono yangu kwako,

nafsi yangu inakuonea kiu kama ardhi kame.

7Ee Mwenyezi Mungu, unijibu haraka,

roho yangu inazimia.

Usinifiche uso wako,

ama sivyo nitafanana na wale wanaoshuka shimoni.

8Asubuhi uniletee neno la upendo wako usiokoma,

kwa kuwa nimeweka tumaini langu kwako.

Nioneshe njia nitakayoiendea,

kwa kuwa kwako nainua nafsi yangu.

9Ee Mwenyezi Mungu, uniokoe na adui zangu,

kwa kuwa nimejificha kwako.

10Nifundishe kufanya mapenzi yako,

kwa maana wewe ndiwe Mungu wangu,

Roho wako mwema na aniongoze

katika nchi tambarare.

11Ee Mwenyezi Mungu, kwa ajili ya jina lako, hifadhi maisha yangu,

kwa haki yako nitoe katika taabu.

12Kwa upendo wako usiokoma,

nyamazisha adui zangu;

waangamize watesi wangu wote,

kwa kuwa mimi ni mtumishi wako.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help