Zaburi 41 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 41Maombi ya mtu mgonjwaKwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.

1Heri mtu yule anayemjali mnyonge,

Mwenyezi Mungu atamwokoa wakati wa shida.

2Mwenyezi Mungu atamlinda na kuyahifadhi maisha yake,

atambariki katika nchi

na hatamwacha katika tamaa ya adui zake.

3Mwenyezi Mungu atamtegemeza akiwa mgonjwa kitandani,

na atamwinua kutoka kitandani mwake.

4Nilisema, “Ee Mwenyezi Mungu nihurumie,

niponye, maana nimekutenda dhambi wewe.”

5Adui zangu wanasema kwa hila,

“Lini atakufa, na jina lake litokomee kabisa.”

6Kila anapokuja mtu kunitazama,

huzungumza uongo,

huku moyo wake ukikusanya masingizio;

kisha huondoka na kuyasambaza.

7Adui zangu wote hunong’onezana dhidi yangu,

hao huniwazia mabaya sana, wakisema,

8“Ugonjwa mbaya sana umempata,

kamwe hatainuka tena kitandani mwake.”

9Hata rafiki yangu wa karibu niliyemwamini,

yule aliyekula chakula changu

ameniinulia kisigino chake.

10Lakini wewe, Ee Mwenyezi Mungu, nihurumie,

ukaniinue tena, ili niweze kuwalipiza kisasi.

11Najua kwamba wapendezwa nami,

kwa kuwa adui yangu hanishindi.

12Katika uadilifu wangu unanitegemeza

na kuniweka kwenye uwepo wako milele.

13Mtukuzeni Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli,

tangu milele na hata milele.

Amen na Amen.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help