Zaburi 96 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 96Mwenyezi Mungu Mfalme mkuu(1 Nyakati 16:23-33)

1Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya;

mwimbieni Mwenyezi Mungu dunia yote.

2Mwimbieni Mwenyezi Mungu, lisifuni jina lake;

tangazeni wokovu wake siku baada ya siku.

3Tangazeni utukufu wake katika mataifa,

matendo yake ya ajabu miongoni mwa mataifa yote.

4Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni mkuu mwenye kustahili kusifiwa kuliko wote;

yeye ni wa kuogopwa kuliko miungu yote.

5Kwa maana miungu yote ya mataifa ni sanamu,

lakini Mwenyezi Mungu aliziumba mbingu.

6Fahari na enzi viko mbele yake;

nguvu na utukufu vimo patakatifu pake.

7Mpeni Mwenyezi Mungu, enyi jamaa za mataifa,

mpeni Mwenyezi Mungu utukufu na nguvu.

8Mpeni Mwenyezi Mungu utukufu unaostahili jina lake;

leteni sadaka na mje katika nyua zake.

9Mwabuduni Mwenyezi Mungu katika uzuri wa utakatifu wake;

dunia yote na itetemeke mbele zake.

10Semeni katika mataifa kwamba, “Mwenyezi Mungu anatawala.”

Ulimwengu ameuweka imara, hauwezi kusogezwa;

atawahukumu watu kwa uadilifu.

11Mbingu na zishangilie, nchi na ifurahi;

bahari na ivume, na vyote vilivyo ndani yake;

12mashamba na yashangilie,

pamoja na vyote vilivyomo.

Kisha miti yote ya msituni itaimba kwa furaha;

13itaimba mbele za Mwenyezi Mungu kwa maana anakuja,

anakuja kuihukumu dunia.

Ataihukumu dunia kwa haki,

na mataifa katika kweli yake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help