Zaburi 35 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 35Kuomba msaada: Kuokolewa kutokana na aduiZaburi ya Daudi.

1Ee Mwenyezi Mungu, pingana na wale wanaopingana nami,

upigane na hao wanaopigana nami.

2Chukua ngao na kigao.

Inuka unisaidie.

3Inua mkuki wako na fumo lako

dhidi ya hao wanaonifuatia.

Iambie nafsi yangu,

“Mimi ni wokovu wako.”

4Wafedheheshwe na waaibishwe

wale wanaotafuta uhai wangu.

Wanaofanya shauri kuniangamiza

wafukuzwe mbali kwa bumbuazi.

5Wawe kama makapi yapeperushwayo na upepo,

malaika wa Mwenyezi Mungu akiwafukuza.

6Njia yao na iwe giza na ya utelezi,

malaika wa Mwenyezi Mungu akiwafuatilia.

7Kwa vile walinifichia wavu wao bila sababu,

na bila sababu wamenichimbia shimo,

8maafa na yawapate ghafula:

wavu walionifichia na uwatege wenyewe,

na waanguke katika shimo hilo,

kwa maangamizi yao.

9Ndipo nafsi yangu itashangilia katika Mwenyezi Mungu

na kuufurahia wokovu wake.

10Nitapaza sauti yangu nikisema,

“Ni nani aliye kama wewe, Ee Mwenyezi Mungu?

Wewe huwaokoa maskini kutokana na wale waliowazidi nguvu,

unawaokoa maskini na wahitaji kutokana na wanaowanyang’anya!”

11Mashahidi wakatili wanainuka,

wananiuliza mambo nisiyoyajua.

12Wananilipa baya kwa jema

na kuiacha nafsi yangu ukiwa.

13Lakini walipokuwa wagonjwa, nilivaa gunia

na nikajinyenyekeza kwa kufunga.

Maombi yangu yaliponirudia bila kujibiwa,

14niliendelea kuomboleza

kama vile wao ni rafiki au ndugu.

Niliinamisha kichwa chini kwa huzuni

kama ninayemwombolezea mama yangu.

15Lakini nilipojikwaa,

walikusanyika kwa shangwe;

washambuliaji walijikusanya dhidi yangu

bila mimi kujua.

Walinisingizia pasipo kukoma.

16Kama watu wasiomcha Mungu, wamenidhihaki,

wamenisagia meno.

17Ee Bwana, utatazama hadi lini?

Niokoe maisha yangu na maangamizi yao,

okoa uhai wangu wa thamani

kutokana na simba hawa.

18Nami nitakushukuru mbele ya kusanyiko kubwa,

nitakusifu katikati ya watu wengi.

19Usiwaache wale wanaonisimanga,

wale ambao ni adui zangu bila sababu;

usiwaache wale ambao ni adui zangu bila sababu

wakonyeze jicho kwa hila.

20Hawazungumzi kwa amani,

bali wanatunga mashtaka ya uongo

dhidi ya wale wanaoishi

kwa utulivu katika nchi.

21Hunifumbulia vinywa vyao wakisema, “Aha! Aha!

Kwa macho yetu wenyewe tumeliona.”

22Ee Mwenyezi Mungu, umeona hili, usiwe kimya.

Usiwe mbali nami, Ee Bwana.

23Amka, inuka unitetee!

Unipiganie Mungu wangu na Bwana wangu.

24Nihukumu kwa haki yako, Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu,

sawasawa na haki yako;

usiwaache wakusimange.

25Usiwaache wafikiri, “Aha, hili ndilo tulilotaka!”

Au waseme, “Tumemmeza.”

26Wote wanaofurahia dhiki yangu

waaibishwe na wachanganyikiwe;

hao wanaojiinua dhidi yangu

wavikwe aibu na dharau.

27Wale wanaofurahia hukumu yangu ya haki

wapige kelele za shangwe na furaha;

hebu waseme siku zote, “Mwenyezi Mungu atukuzwe,

ambaye amefurahia mafanikio ya mtumishi wake.”

28Ulimi wangu utanena haki yako

na sifa zako mchana kutwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help