Mika 4 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Mlima wa Mwenyezi Mungu(Isaya 2:2-4)

1Katika siku za mwisho

mlima wa Hekalu la Mwenyezi Mungu utaimarishwa

kama mlima mkuu miongoni mwa milima yote;

utainuliwa juu ya vilima,

na watu wa mataifa watamiminika humo.

2Mataifa mengi yatakuja na kusema,

“Njooni, twendeni kwenye mlima wa Mwenyezi Mungu,

kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo.

Atatufundisha njia zake,

ili tuweze kuenenda katika mapito yake.”

Torati itatoka Sayuni,

neno la Mwenyezi Mungu litatoka Yerusalemu.

3Atahukumu kati ya mataifa mengi,

na ataamua migogoro ya mataifa

yenye nguvu na yaliyo mbali.

Watafua panga zao ziwe majembe,

na mikuki yao kuwa miundu ya kukata matawi.

Taifa halitainua upanga dhidi ya taifa jingine,

wala hawatajifunza vita tena.

4Kila mtu ataketi chini ya mzabibu wake

na chini ya mtini wake,

wala hakuna mtu atakayewaogopesha,

kwa kuwa Mwenyezi Mungu,

Mungu wa majeshi ya mbinguni amesema.

5Mataifa yote yanaweza kutembea

katika jina la miungu yao;

sisi tutatembea katika jina la Mwenyezi Mungu,

Mungu wetu milele na milele.

Mpango wa Mwenyezi Mungu

6“Katika siku hiyo,” asema Mwenyezi Mungu,

“nitawakusanya walemavu;

nitawakusanya walio uhamishoni

na wale niliowahuzunisha.

7Nitawafanya walemavu kuwa mabaki,

wale waliofukuzwa kuwa taifa lenye nguvu.

Mwenyezi Mungu atawatawala katika Mlima Sayuni

kuanzia siku hiyo na hata milele.

8Lakini kwako wewe, ee mnara wa ulinzi wa kundi,

ee ngome ya Binti Sayuni,

milki ya awali itarudishwa kwako,

ufalme utakuja kwa Binti Yerusalemu.”

9Kwa nini sasa unalia kwa nguvu:

kwani huna mfalme?

Je, mshauri wako amekufa, hata maumivu yakukamate

kama ya mwanamke

aliye na uchungu wa kuzaa?

10Gaagaa kwa uchungu, ee Binti Sayuni,

kama mwanamke mwenye uchungu wa kuzaa,

kwa kuwa sasa ni lazima uuache mji

ukapige kambi uwanjani.

Utaenda Babeli;

huko utaokolewa.

Huko Mwenyezi Mungu atakukomboa

kutoka mikononi mwa adui zako.

11Lakini sasa mataifa mengi

yamekusanyika dhidi yako.

Wanasema, “Mwache anajisiwe,

macho yetu na yatazame Sayuni kwa furaha!”

12Lakini hawayajui

mawazo ya Mwenyezi Mungu;

hawauelewi mpango wake,

yeye awakusanyaye kama miganda

kwenye sakafu ya kupuria.

13“Inuka upure, ee Binti Sayuni,

kwa kuwa nitakupa pembe za chuma;

nitakupa kwato za shaba

na utavunja vipande vipande mataifa mengi.”

Utatoa mapato yao waliopata kwa udanganyifu kwa Mwenyezi Mungu,

utajiri wao kwa Bwana wa dunia yote.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help