Zaburi 40 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 40Wimbo wa sifaKwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.

1Nilimngoja Mwenyezi Mungu kwa saburi,

naye akanijia na kusikia kilio changu.

2Akanipandisha kutoka shimo la uharibifu,

kutoka matope na utelezi;

akaiweka miguu yangu juu ya mwamba

na kunipa mahali imara pa kusimama.

3Akaweka wimbo mpya kinywani mwangu,

wimbo wa sifa kwa Mungu wetu.

Wengi wataona na kuogopa

na kuweka tumaini lao kwa Mwenyezi Mungu.

4Heri mtu yule amfanyaye Mwenyezi Mungu kuwa tumaini lake,

asiyewategemea wenye kiburi,

wale wenye kugeukia miungu ya uongo.

5Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu,

umefanya mambo mengi ya ajabu.

Mambo uliyopanga kwa ajili yetu

hakuna awezaye kukuhesabia;

kama ningesema na kuyaelezea,

yangekuwa mengi mno kuyatangaza.

6Dhabihu na sadaka hukuvitaka,

lakini umefungua masikio yangu;

sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi

hukuzihitaji.

7Ndipo niliposema, “Mimi hapa, nimekuja:

imeandikwa kunihusu katika kitabu.

8Ee Mungu wangu,

natamani kuyafanya mapenzi yako;

sheria yako iko ndani ya moyo wangu.”

9Nimehubiri haki katika kusanyiko kubwa,

sikufunga mdomo wangu,

Ee Mwenyezi Mungu, kama ujuavyo.

10Sikuficha haki yako moyoni mwangu;

ninasema juu ya uaminifu wako na wokovu wako.

Sikuficha upendo wako na kweli yako

mbele ya kusanyiko kubwa.

11Ee Mwenyezi Mungu, usinizuilie huruma zako,

upendo wako na kweli yako daima vinilinde.

12Kwa maana taabu zisizohesabika zimenizunguka,

dhambi zangu zimenikamata, hata nisiweze kuona.

Zimekuwa nyingi kuliko nywele za kichwa changu,

nao moyo unazimia ndani yangu.

13Ee Mwenyezi Mungu, uwe radhi kuniokoa;

Ee Mwenyezi Mungu, njoo hima unisaidie.

14Wote wanaotafuta kuniua,

waaibishwe na kufadhaishwa;

wote wanaotamani kuangamizwa kwangu,

wafukuzwe mbali kwa aibu.

15Wale wanaoniambia, “Aha! Aha!”

wafadhaishwe na iwe aibu yao.

16Lakini wote wanaokutafuta

washangilie na kukufurahia,

wale wanaoupenda wokovu wako siku zote waseme,

“Mwenyezi Mungu atukuzwe!”

17Lakini mimi bado ni maskini na mhitaji;

Bwana na anifikirie.

Wewe ndiwe msaada wangu na Mwokozi wangu;

Ee Mungu wangu, usikawie.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help