Zaburi 49 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Zaburi 49Upumbavu wa kutegemea maliKwa mwimbishaji. Zaburi ya wana wa Kora.

1Sikieni haya, enyi mataifa yote,

sikilizeni, ninyi wote mnaoishi dunia hii.

2Wakubwa kwa wadogo,

matajiri na maskini pamoja:

3Kinywa changu kitasema maneno ya hekima,

usemi wa moyo wangu utatoa ufahamu.

4Nitatega sikio langu nisikilize mithali,

nitafafanua kitendawili kwa zeze:

5Kwa nini niogope siku mbaya zinapokuja,

wakati wadanganyifu waovu wanaponizunguka,

6wale wanaotegemea mali yao

na kujivunia utajiri wao mwingi?

7Hakuna mwanadamu yeyote

awezaye kuukomboa uhai wa mwingine,

au kumpa Mungu fidia kwa ajili yake.

8Fidia ya uhai ni gharama kubwa,

hakuna malipo yoyote yanayotosha,

9ili aishi milele

na asione uharibifu.

10Wote wanaona kwamba watu wenye hekima hufa;

wajinga na wapumbavu vivyo hivyo huangamia

na kuwaachia wengine mali yao.

11Makaburi yao yatabaki kuwa nyumba zao za milele,

makao yao vizazi vyote;

ingawa walikuwa na mashamba

na kuyaita kwa majina yao.

12Lakini mwanadamu, licha ya utajiri wake, hadumu;

anafanana na mnyama aangamiaye.

13Hii ndiyo hatima ya wale wanaojitumainia wenyewe,

pia ya wafuasi wao, waliothibitisha misemo yao.

14Kama kondoo, wamewekewa kwenda kaburini,

nacho kifo kitawala.

Wanyofu watawatawala asubuhi,

maumbile yao yataozea kaburini,

mbali na majumba yao makubwa ya fahari.

15Lakini Mungu atakomboa uhai wangu dhidi ya kaburi;

hakika atanichukua kwake.

16Usitishwe mtu anapotajirika,

fahari ya nyumba yake inapoongezeka,

17kwa maana hatachukua chochote atakapokufa,

fahari yake haitashuka pamoja naye.

18Ingawa alipokuwa akiishi alijihesabu kuwa heri,

na wanadamu wanakusifu unapofanikiwa,

19atajiunga na kizazi cha baba zake,

ambao hawataona kamwe nuru ya uzima.

20Wanadamu wenye utajiri bila ufahamu

ni kama wanyama wanaoangamia.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help