Nahumu 3 - Kiswahili Contemporary Scriptures 2024

Ole wa Ninawi

1Ole wa mji unaomwaga damu,

uliojaa uongo,

uliojaa nyara,

na usiokosa mateka.

2Kelele za mijeledi,

vishindo vya magurudumu,

farasi wanaoenda mbio

na mshtuo wa magari ya vita!

3Wapanda farasi wanaenda mbio,

panga zinametameta,

na mikuki inang’aa!

Majeruhi wengi,

malundo ya maiti,

idadi ya miili isiyohesabika,

watu wanajikwaa juu ya mizoga:

4haya yote kwa sababu ya wingi wa tamaa za kahaba,

anayeshawishi, bibi mkuu wa mambo ya uchawi,

anayewatia utumwani mataifa kwa ukahaba wake

na pia jamaa za watu kwa ulozi wake.

5Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni anasema,

“Mimi ni kinyume na ninyi.

Nitafunika uso wako kwa gauni lako.

Nitaonesha mataifa uchi wako

na falme aibu yako.

6Nitakutupia uchafu,

nitakufanyia dharau

na kukufanya kioja.

7Wote wanaokuona watakukimbia na kusema,

‘Ninawi inaangamia,

nani atakayeomboleza kwa ajili yake?’

Nitampata wapi yeyote wa kukufariji?”

8Je, wewe ni bora kuliko No-Amoni,

uliopo katika Mto Naili,

uliozungukwa na maji?

Mto ulikuwa kinga yake,

nayo maji yalikuwa ukuta wake.

9Kushi na Misri walikuwa nguvu zake zisizo na mpaka;

Putu na Libia walikuwa miongoni mwa wale walioungana naye.

10Hata hivyo alichukuliwa mateka

na kwenda uhamishoni.

Watoto wake wachanga walivunjwa vunjwa vipande

kwenye mwanzo wa kila barabara.

Kura zilipigwa kwa watu wake wenye heshima,

na watu wake wote wakuu walifungwa kwa minyororo.

11Wewe pia utalewa;

utaenda mafichoni

na kutafuta kimbilio kutoka kwa adui.

12Ngome zako zote ni kama mitini

yenye matunda yake ya kwanza yaliyoiva;

wakati inapotikiswa,

tini huanguka kwenye kinywa chake alaye.

13Tazama vikosi vyako:

wote ni wanawake!

Malango ya nchi yako

yamekuwa wazi kwa adui zako;

moto umeteketeza mapingo yake.

14Teka maji kwa ajili ya kuzingirwa kwako,

imarisha ulinzi wako,

Ufanyie udongo wa mfinyanzi kazi,

yakanyage matope,

karabati tanuru la kuchomea matofali!

15Huko moto utakuteketeza,

huko upanga utakuangusha chini

na kama vile panzi, watakumaliza.

Ongezeka kama panzi,

ongezeka kama nzige!

16Umeongeza idadi ya wafanyabiashara wako

hata wamekuwa wengi kuliko nyota za angani,

lakini kama nzige wanaacha nchi tupu

kisha huruka na kwenda zake.

17Walinzi wako ni kama nzige,

maafisa wako kama makundi ya nzige

wanaotua kwenye kuta wakati wa siku ya baridi;

lakini wakati jua linapotokea wanaruka kwenda zao,

na hakuna anayejua wanakoenda.

18Ee mfalme wa Ashuru, wachungaji wako wanasinzia;

wakuu wako wanalala chini mavumbini kupumzika.

Watu wako wametawanyika juu ya milima

bila kuwa na mtu yeyote wa kuwakusanya.

19Hakuna kitu kinachoweza kuponya jeraha lako;

jeraha lako ni la kukuua.

Kila anayesikia habari zako,

hupiga makofi kwa kuanguka kwako,

kwa kuwa ni nani ambaye hajaguswa

na ukatili wako usio na mwisho?

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help