Wimbo 6 - Kiswahili Contemporary Version (Neno: Bibilia Takatifu) 2025

Rafiki

1Mpenzi wako ameenda wapi,

ewe mzuri kupita wanawake wote?

Mpenzi wako amegeukia njia ipi,

tupate kumtafuta pamoja nawe?

Mpendwa

2Mpenzi wangu ameenda bustanini mwake,

kwenye vitalu vya vikolezo,

kujilisha bustanini

na kukusanya yungiyungi.

3Mimi ni wake mpenzi wangu,

na mpenzi wangu ni wangu;

yeye hujilisha kati ya yungiyungi.

Mpenzi

4Wewe ni mzuri, mpendwa wangu, kama Tirsa,

unapendeza kama Yerusalemu,

umetukuka kama jeshi lenye bendera.

5Uyageuze macho yako mbali nami;

yananigharikisha.

Nywele zako ni kama kundi la mbuzi

wanaoteremka kutoka Gileadi.

6Meno yako ni kama kundi la kondoo

wanaotoka kuogeshwa.

Kila mmoja ana pacha lake,

hakuna hata mmoja aliye peke yake.

7Mashavu yako nyuma ya shela yako

ni kama vipande viwili vya komamanga.

8Panaweza kuwa na malkia sitini,

masuria themanini,

na mabikira wasiohesabika;

9lakini hua wangu, mkamilifu wangu,

ni wa namna ya pekee,

binti pekee kwa mama yake,

kipenzi cha yeye aliyemzaa.

Wanawali walimwona na kumwita aliyebarikiwa;

malkia na masuria walimsifu.

Rafiki

10Ni nani huyu atokeaye kama mapambazuko,

mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua,

ametukuka kama nyota zinazofuatana?

Mpenzi

11Niliteremka kwenye bustani ya miti ya milozi

ili kutazama machipuko ya bondeni,

kuona kama mizabibu imechipua

au kama mikomamanga imechanua maua.

12Kabla sijangʼamua,

shauku yangu iliniweka

katikati ya magari ya vita ya wakuu wangu.

Rafiki

13Rudi, rudi, ee Mshulami;

rudi, rudi ili tupate kukutazama!

Mpenzi

Kwa nini kumtazama Mshulami,

kama kutazama ngoma ya Mahanaimu?

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help