Zaburi 66 - Kiswahili Contemporary Version (Neno: Bibilia Takatifu) 2025

Zaburi 66Kusifu Mungu kwa ajili ya wema wakeKwa mwimbishaji. Wimbo. Zaburi.

1Mpigieni Mungu kelele za shangwe, dunia yote!

2Imbeni utukufu wa jina lake;

mpeni sifa zake kwa utukufu!

3Mwambieni Mungu, “Jinsi gani

yalivyo ya kutisha matendo yako!

Uwezo wako ni mkuu mno kiasi kwamba

adui wanajikunyata mbele zako.

4Dunia yote yakusujudia,

wanakuimbia wewe sifa,

wanaliimbia sifa jina lako.”

5Njooni mwone yale Mungu aliyoyatenda,

mambo ya kutisha aliyoyatenda

miongoni mwa wanadamu!

6Alifanya bahari kuwa nchi kavu,

wakapita kati ya maji kwa miguu,

njooni, tumshangilie.

7Yeye hutawala kwa uwezo wake milele,

macho yake huangalia mataifa yote:

waasi wasithubutu kujiinua dhidi yake.

8Enyi mataifa, msifuni Mungu wetu,

sauti ya sifa yake isikike,

9ameyahifadhi maisha yetu

na kuizuia miguu yetu kuteleza.

10Ee Mungu, wewe ulitujaribu,

ukatusafisha kama fedha.

11Umetuingiza kwenye nyavu

na umetubebesha mizigo mizito

migongoni mwetu.

12Uliwaruhusu watu watukalie vichwani,

tulipita kwenye moto na kwenye maji,

lakini ulituleta kwenye nchi

iliyojaa utajiri tele.

13Nitakuja hekaluni mwako na sadaka za kuteketezwa

na kukutimizia nadhiri zangu:

14nadhiri ambazo midomo yangu iliahidi

na nilizotamka kwa kinywa changu

nilipokuwa katika shida.

15Nitakutolea dhabihu za wanyama wanono

na sadaka za kondoo dume,

nitakutolea mafahali na mbuzi.

16Njooni msikilize ninyi nyote mnaomcha Mungu,

nami niwaambie aliyonitendea.

17Nilimlilia kwa kinywa changu,

sifa zake zilikuwa katika ulimi wangu.

18Kama ningekuwa nimeyaficha maovu moyoni mwangu,

Bwana asingekuwa amenisikiliza;

19lakini hakika Mungu amenisikiliza

na amesikia sauti yangu katika maombi.

20Ahimidiwe Mungu,

ambaye hakulikataa ombi langu,

wala kunizuilia upendo wake!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help