Hesabu 34 - Kiswahili Contemporary Version (Neno: Bibilia Takatifu) 2025

Mipaka ya Kanaani

1 Bwana akamwambia Musa,

2“Waamuru Waisraeli na uwaambie: ‘Mtakapoingia nchi ya Kanaani, nchi ambayo itagawanywa kwenu kama urithi itakuwa na mipaka ifuatayo:

3“ ‘Upande wenu wa kusini utajumuisha sehemu ya Jangwa la Sini kufuata mpaka wa Edomu. Upande wa mashariki mpaka wenu wa kusini utaanzia mwisho wa Bahari ya Chumvi,

4katiza kusini mwa Pito la Akrabimu, kuendelea hadi Sini na kwenda kusini mwa Kadesh-Barnea. Kisha mpaka huo utaenda hadi Hasar-Adari hadi Azmoni,

5mahali mpaka utapinda, na kuunganika na Kijito cha Misri, na kumalizikia kwenye Bahari ya Kati.

6Mpaka wenu wa magharibi utakuwa Bahari ya Kati. Huu utakuwa mpaka wenu upande wa magharibi.

7Kwa mpaka wenu wa kaskazini, wekeni alama kuanzia Bahari ya Kati hadi mlima Hori,

8na kutoka mlima Hori hadi Pito la Hamathi. Kisha mpaka utaenda hadi Sedadi,

9kuendelea hadi Zifroni, na kuishia Hasar-Enani. Huu utakuwa mpaka wenu upande wa kaskazini.

10Kwa mpaka wenu wa mashariki, wekeni alama kuanzia Hasar-Enani hadi Shefamu.

11Mpaka utaelekea kusini kuanzia Shefamu hadi Ribla upande wa mashariki wa Aini, na kuendelea kwenye miteremko mashariki mwa Bahari ya Kinerethi.

12Kisha mpaka utashuka kuelekea Mto Yordani na kuishia katika Bahari ya Chumvi.

“ ‘Hii itakuwa nchi yenu, ikiwa na mipaka yake kila upande.’ ”

13Musa akawaamuru Waisraeli: “Gawanyeni nchi hii kwa kura kama urithi. Bwana ameagiza kwamba itolewe kwa yale makabila tisa na nusu,

14kwa sababu jamaa ya kabila la Reubeni, kabila la Gadi, na nusu ya kabila la Manase wamekwishapokea urithi wao.

15Haya makabila mawili na nusu wamekwishapokea urithi wao upande wa mashariki wa Yordani ngʼambo ya Yeriko, kuelekea mawio ya jua.”

16 Bwana akamwambia Musa,

17“Haya ndiyo majina ya watu ambao watakusaidia kugawanya nchi kama urithi: Eleazari kuhani na Yoshua mwana wa Nuni.

18Tena uteue kiongozi mmoja kutoka kila kabila kusaidia kuigawanya nchi.

19“Haya ndiyo majina yao:

“Kalebu mwana wa Yefune, kutoka kabila la Yuda;

20Shemueli mwana wa Amihudi, kutoka kabila la Simeoni;

21Elidadi mwana wa Kisloni, kutoka kabila la Benyamini;

22Buki mwana wa Yogli, kiongozi kutoka kabila la Dani;

23Hanieli mwana wa Efodi, kiongozi kutoka kabila la Manase mwana wa Yusufu;

24Kemueli mwana wa Shiftani, kiongozi kutoka kabila la Efraimu mwana wa Yusufu;

25Elisafani mwana wa Parnaki, kiongozi kutoka kabila la Zabuloni;

26Paltieli mwana wa Azani, kiongozi kutoka kabila la Isakari;

27Ahihudi mwana wa Shelomi, kiongozi kutoka kabila la Asheri;

28Pedaheli mwana wa Amihudi, kiongozi kutoka kabila la Naftali.”

29Hawa ndio watu ambao Bwana aliamuru wagawanye urithi kwa Waisraeli katika nchi ya Kanaani.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help