Zaburi 85 - Kiswahili Study Bible

Kuliombea fanaka taifa(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Wakorahi)

1Ee Mwenyezi-Mungu,

umeifadhili nchi yako;

umemjalia Yakobo bahati nzuri tena.

2Umewasamehe watu wako kosa lao;

umezifuta dhambi zao zote.

3Umeizuia ghadhabu yako yote;

umeiacha hasira yako kali.

4Uturekebishe tena, ee Mungu mwokozi wetu;

uiondoe chuki uliyo nayo juu yetu.

5Je, utatukasirikia hata milele?

Je, utadumisha ghadhabu yako kwa vizazi vyote?

6Je, hutatujalia tena maisha mapya,

ili watu wako wafurahi kwa sababu yako?

7Utuoneshe, fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu,

utujalie wokovu wako.

8Hebu nisikie anachosema Mwenyezi-Mungu;

maana anaahidi kuwapa watu wake amani,

watu wake mwenyewe wasiporudia upuuzi wao

9Hakika yu tayari kuwaokoa wanaomheshimu,

na utukufu wake utadumu nchini mwetu.

10Fadhili zake na uaminifu vitakutana;

uadilifu na amani vitaungana.

11Uaminifu utachipuka katika nchi;

uadilifu utashuka toka mbinguni.

12Naam, Mwenyezi-Mungu atatuletea fanaka,

na nchi yetu itatoa mazao yake mengi.

13Uadilifu utamtangulia Mungu

na kumtayarishia njia yake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help