Zaburi 97 - Swahili Common Language DC Bible

Mungu mtawala mkuu

1Mwenyezi-Mungu anatawala!

Furahi, ee dunia!

Furahini enyi visiwa vingi!

2Mawingu na giza nene vyamzunguka;

uadilifu na haki ni msingi wa utawala wake.

3Moto watangulia mbele yake,

na kuwateketeza maadui zake pande zote.

4Umeme wake wauangaza ulimwengu;

dunia yauona na kutetemeka.

5Milima yayeyuka kama nta mbele ya Mwenyezi-Mungu;

naam, mbele ya Bwana wa dunia yote.

6Mbingu zatangaza uadilifu wake;

na mataifa yote yauona utukufu wake.

7Wote wanaoabudu sanamu wanaaibishwa,

naam, wote wanaojisifia miungu duni;

miungu yote husujudu mbele zake.

8Watu wa Siyoni wanafurahi;

watu wa Yuda wanashangilia,

kwa sababu ya hukumu zako, ee Mungu.

9Wewe Mwenyezi-Mungu ni mkuu juu ya dunia yote;

wewe watukuka juu ya miungu yote.

10Mwenyezi-Mungu huwapenda wanaochukia uovu,

huyalinda maisha ya watu wake;

huwaokoa makuchani mwa waovu.

11Mwanga humwangazia mtu mwadilifu,

na furaha kwa watu wanyofu wa moyo.

12Furahini kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu;

mshukuruni kwa ajili ya jina lake takatifu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help