Zaburi 46 - Swahili, Common Language Bible

Mungu yuko upande wetu(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Wakorahi. Mtindo wa Alamothi)

1Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu;

yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu.

2Kwa hiyo hatutaogopa chochote,

dunia ijapoyeyuka

na milima kutikisika kutoka baharini;

3hata kama bahari ikichafuka na kutisha,

na milima ikatetemeka kwa machafuko yake.

4Kuna mto ambao maji yake hufurahisha mji wa Mungu,

makao matakatifu ya Mungu Mkuu.

5Mungu yumo mjini humo, nao hauwezi kutikiswa;

Mungu ataupa msaada alfajiri na mapema.

6Mataifa yaghadhibika na tawala zatikisika;

Mungu anguruma nayo dunia yayeyuka.

7Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi,

Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.

8Njoni mwone matendo ya Mwenyezi-Mungu;

oneni maajabu aliyoyafanya duniani.

9Hukomesha vita popote duniani,

huvunjavunja pinde na mikuki,

nazo ngao huziteketeza.

10Asema: “Nyamazeni na kujua kuwa mimi ni Mungu!

Mimi natukuka katika mataifa yote;

mimi natukuzwa ulimwenguni kote!”

11Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi,

Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help