Zaburi 30 - Swahili, Common Language Bible

Sala ya shukrani(Zaburi ya Daudi)

1Ee Mwenyezi-Mungu, nakutukuza maana umeniokoa,

wala hukuwaacha maadui zangu wanisimange.

2Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu,

nilikulilia msaada, nawe ukaniponya.

3Ee Mwenyezi-Mungu, umeniokoa kutoka kuzimu;

umenipa tena uhai,

umenitoa miongoni mwa waendao kuzimu.

4Mwimbieni Mwenyezi-Mungu sifa, enyi waaminifu wake;

kumbukeni utakatifu wake na kumshukuru.

5Hasira yake hudumu kitambo kidogo,

wema wake hudumu milele.

Kilio chaweza kuwapo hata usiku,

lakini asubuhi huja furaha.

6Mimi nilipofanikiwa, nilisema:

“Kamwe sitashindwa!”

7Kwa wema wako, ee Mwenyezi-Mungu,

umeniimarisha kama mlima mkubwa.

Lakini ukajificha mbali nami,

nami nikafadhaika.

8Nilikulilia wewe, ee Mwenyezi-Mungu;

naam niliomba dua kwako ee Mwenyezi-Mungu:

9“Je, utapata faida gani nikifa

na kushuka hadi kwa wafu?

Je, mavumbi ya wafu yanaweza kukusifu?

Je, yanaweza kusimulia uaminifu wako?

10Usikie, ee Mwenyezi-Mungu, unihurumie;

ee Mwenyezi-Mungu, unisaidie!”

11Wewe umegeuza maombolezo langu kuwa ngoma ya furaha;

umeniondolea huzuni yangu, ukanizungushia furaha.

12Mimi nitakusifu wala sitakaa kimya.

Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu nitakushukuru milele.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help